TANESCO SACCOS YAIGUSA SEKTA YA AFYA KWA KUTOA MASHUKA YENYE THAMANI YA MILIONI 23 JIJINI DODOMA

Na. Janeth Raphael, MichuziTv -Dodoma 

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amesema pamoja serikali kufanya kazi kubwa hasa katika Sekta ya Afya ikiwemo ununuzi wa vifaa, Dawa, Majengo na miundombinu na watumishi lakini bado safari ya maendeleo katika sekta hiyo huwa haiishi kutokana na watu kuongezeka na magonjwa kubadilika.




RC Senyamule alisema hayo jijini Dodoma katika hafla fupi ya kupokea Mashuka 300 ya kuhudumia wagonjwa waliopo katika hospitali za Mkoa wa Dodoma yaliyotolewa na wana Ushirika wa Tanesco Saccos. 

Alisema kuwa kutoka na uhitaji wa kila siku serikali hata kama ingenunua mashuka mengi kiasi gani bado yasingeweza kudumu siku zote kwasababu ingefika muda yangechakaa na kuhitajika mengine.

“Tunajua kuwa serikali yetu chini ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia imefanya kazi kubwa sana katika Sekta ya Afya. Zipo sekta nyingine lakini katika sekta ya Afya imefanya makubwa kuanzia Vifaa,Majengo,Miundombinu,Watumishi na vitu vingine vingi, lakini tunafahamu kuwa bado safari hii ya maendeleo haina mwisho kila siku tunafanya lakini bado watu wanaongezeka na magonjwa yanabadilika kupelekea uhitaji wa kila siku katika baadhi ya maeneo. Kwahiyo, mahitaji hayafiki mwisho hata siku moja. Hivyo, ukienda kwenye sekta ya Afya unakuta kuna uhitaji mpya, mfano mashuka hata serikali ikinunua mengi kiasi gani lakini baada ya muda yachakaa na kuhitajika mengine” alisema Senyamule.

Aidha, aliipongeza Tanesco Saccos kwa mchango huo wa mashuka ambao ni wa thamani na heshima kwa wana Dodoma utakaowagusa wagonjwa ambao watafika katika Hospitali za Mkoa wa Dodoma ambazo zitapewa mashuka hayo ambayo yataleta kumbukumbu nzuri, kwasababu fedha zilizotakiwa kununua mashuka katika hospitali hizo sasa zitakwenda kununua Dawa na vifaa vingine.

Naye Mtendaji Mkuu wa Tanesco Saccos, Andrea Hilary alisema kuwa katika zoezi hilo la kutoa mahitaji ya mashuka katika hospitali walipata msukumo kwa kujua kuwa sekta ya Afya ni kubwa na yenye uhitaji mwingi. Hivyo, serikali pekee haiwezi kujitosheleza pamoja na kufanya makubwa katika sekta hiyo, kwasababu uhitaji ni wakila siku na kwa kuona hilo na wao waliona wanayo nafasi ya kufanya ili kuigusa jamii.

Alisema kuwa walichagua eneo hilo la kusambaza mashuka baada ya wao kupata elimu kuwa kitanda kimoja kinahitaji mashuka nane kwa siku ili kukamilisha mzunguko wa mgonjwa kulala katika mazingira ambayo ni safi na salama. Hivyo, katika mipango yao ya mwaka wakaona waguse eneo hilo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tanesco Saccos, Omary Shabani alieleza kuwa wameona ni muhimu kujikita katika sekta ya Afya ambapo wamechangia mashuka 1,300 katika sekta nzima ya Afya na kwa Mkoa wa Dodoma wametoa mashuka 300 yenye thamani ya shilingi milioni 23, hiyo yote ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutatua changamoto zinazoikabiki sekta ya Afya.

Pamoja na kuahidi kuendelea kuifikia mikoa mingine kwasababu ni awamu ya pili ambapo awamu ya kwanza walitoa mashuka yenye thamani ya shilingi milioni 88, mashuka takribani 1,500 na awamu hii ya pili wameanza na mashuka 1,300.

Mashuka haya yaliyopokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ni Mashuka 300 yenye thamani ya shilingi milioni 23 ambayo yatagwanywa katika wilaya zote.

 Chanzo: MICHUZI BLOG  

Comments

Popular Posts

MAKAMU WA RAIS ASHIRIKI MISA TAKATIFU YA UPADIRISHO JIMBO KATOLIKI DODOMA

TANZANIA YAENDELEA KUTANGAZA NA KUKUZA KISWAHILI NA UTAMADUNI WAKE KIMATAIFA