MAWAKILI NCHINI WATAKIWA KWENDA KUZISOMA SHERIA ZA UCHAGUZI MKUU

Na. Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma


Mawakili nchini Tanzania wametakiwa kwenda kuzisoma sheria za Uchaguzi Mkuu, ili waweze kuwasaidia kujaza fomu wagombea waliojitokeza kutia nia, lakini pia kutatua migogoro itakayowasilishwa kwa kukosa uelewa katika Mahakama mbalimbali hapa nchini.


Jaji Mkuu wa Tanzania ,George Masaju aliyasema hayo jijini Dodoma wakati akiwathibitisha na kuwapokea Mawakili 449 wakiwemo wa Serikali na wa kujitegemea, ikiwemo kuorodheshwa rasmi katika orodha ya mawakili waliothibitishwa hapa nchini.


Aidha, aliwataka Mawakili hao kwenda kufanya kazi katika mikoa mingine tofauti na Dar es Salaam na Dodoma ambayo ina mawakili wa kutosha, ili kuepuka kuitwa vishoka hasa ukizingatia soko la Kada hiyo ni kubwa kwa sasa.

Alisema kuwa kuna sheria nyingi zikiwemo za Polisi, Uchaguzi na nyingine. Na kusema kuwa Mawakili wanapaswa kutumia muda mwingi kuzisoma na kuzielewa ili waweze kutumia fursa ya kuwasaidia wagombea mbalimbali waliojitokeza kuchukua fomu za kugombea nafasi za uongozi. “Najua kazi zetu nyingi tunazipata kupitia kutatua migogoro mbalimbali. Hivyo, tuweke jitihada ya kuzisoma sheria ili tuzielewe maana kuthibitishwa, kupewa vyeti na utendaji ni vitu viwili tofauti” alisema Jaji Mkuu Masaju.

Vilevile, aliwataka Mawakili kwenda kukiishi kiapo walichoapa na kukifanyia kazi ipasavyo, wasome sheria kila mara kwa sababu hubadilika, ili waweze kuisaidia jamii kwa ujumla katika maeneo ambayo watakwenda kuwajibika hapa nchini. “Sisi tuliojaa hapa wakati mnapewa kiapo hatujaja kuwashangilia tumekuja kushuhudia kiapo chenu kama mtakwenda kukiishi kama Sheria inavyoelekeza” alisema.

Jaji Mkuu akizungumzia kuhusiana na Mawakili hao kupenda kuishi kwenye miji mikubwa kama Dar es Salaam na Dodoma, alisema kitendo hicho kinamchukiza sana kwa sababu kuna maeneo mengi ambayo yana migogoro na kuwataka waende sehemu hizo wakawatumikie wananchi.

Akitolea mfano Wilaya ya Kilombero ambako kuna mashamba ya miwa, kuna wakulima wengi pamoja na jamii ambayo inahitaji huduma ya sheria, hivyo, waende huko kuwatumikia wananchi badala ya kubaki kwenye miji mikubwa. “Nisingependa kuona mnazunguka Dar es Salaam na Dodoma muonekane kama vishoka, tawanyikeni mikoa mingine mkafanye kazi ya kutenda haki ili kuisaidia jamii, lakini sitaki kusikia mnauza utu wenu kwa kupewa fedha badala ya kutenda haki” alisema Jaji Mkuu.

Alisema kuwa wasitegemee kwenda kuishi kama wanasiasa wao wanapaswa kwenda kutenda haki ili kuendelea kuaminika mbele ya jamii na kuongeza kuwa kama kesi haiwezi anapaswa kumwambia mteja wake ukweli na sio kuchukua pesa yake bure. “Msitende dhambi ya kuchukua fedha ya watu ilihali mnajua kesi huiwezi ni bora umwambie ukweli mteja, usiwaze kununua gari ndogo kwa pesa ya mteja ambayo unajua kesi hashindi, hata wewe hutafanikiwa kwa sababu hujui amehangaika vipi kuitafuta hiyo pesa ili akulipe” alisema.

Naye Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Chiganga Tengwa alisoma idadi ya mawakili waliopokelewa na kuthibitishwa huku akiwataka kufuata taratibu watakazoelekezwa.

Ongezeko la idadi hiyo ya Mawakili waliothibitishwa imefanya kufikia mawakili 13,446 ambao watakuwa wanafanya shughuli za uwakili katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Chanzo: MICHUZI BLOG  

 

Comments

Popular Posts

MAKAMU WA RAIS ASHIRIKI MISA TAKATIFU YA UPADIRISHO JIMBO KATOLIKI DODOMA

TANZANIA YAENDELEA KUTANGAZA NA KUKUZA KISWAHILI NA UTAMADUNI WAKE KIMATAIFA