Mtendaji Kata Nkuhungu anena fursa kongamano la vijana

Na. Dennis Gondwe, NKUHUNGU

Kongamano la vijana ni fursa ya kuwakutanisha vijana wa Kata ya Nkuhungu na wenzao kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Dodoma kujadili fursa zilizopo na jinsi ya kuzifikia kwa ajili ya kujiletea maendeleo.

Afisa Mtendaji wa Kata ya Nkuhungu, Mwasiti Migilla akiwa katika moja ya majukumu yake



Baadhi ya washiriki wa kongamano la vijana Wilaya ya Dodoma


Kauli hiyo ilitolewa na Afisa Mtendaji wa Kata ya Nkuhungu, Mwasiti Migilla alipokuwa akiwapokea vijana wanaohuduria kongamano la vijana linalofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Nkuhungu jijini Dodoma likienda sambamba na mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2024 wilayani Dodoma.

Migilla alisema kuwa kata yake imepata heshima ya kuwa mwenyeji wa kongamano la vijana na mkesha wa Mwenge wa Uhuru mwaka 2024 katika Wilaya ya Dodoma. “Matukio haya mawili ni makubwa na ni heshima kubwa kwetu wananchi wa Kata ya Nkuhungu. Vijana wanapata fursa ya kubadilishana mawazo na uzoefu pamoja na kujadili fursa mbalimbali zilizopo katika wilaya yao kwa lengo la kuzifikia na kujiletea maendeleo” alisema Migilla.

Akiongelea mkesha wa Mwenge wa Uhuru mwaka 2024, alisema kuwa wananchi wa Kata ya Nkuhungu ni wafuasi wa Mwenge wa Uhuru tangu miaka ya nyuma. “Kata ya Nkuhungu huwa tunakesha na Mwenge wa Uhuru, yaani huwa hakuna kulala. Nitumie fursa hii kuwaalika wananchi wote wa Nkuhungu na maeneo mengine ya Wilaya ya Dodoma kujitokeza kwa wingi kwenye mkesha. Kutakuwa na burudani zinazogusa makundi yote hivyo, hii siyo ya kusimuliwa” Migilla.

Kwa upande wake mshiriki wa kongamano la vijana, Msifuni Mwasi alisema kuwa kongamano hilo ni muhimu kwa sababu linawakutanisha vijana wengi kwa pamoja ili kuweza kujadili fursa na changamoto zao. Aidha, alishauri makongamano kama hayo yawe yanafanyika mara kwa mara yakigusa na vijana wa maeneo ya pembezoni.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma