Msalato Sekondari wamshukuru Rais, Dkt. Samia ujenzi wa mabweni

 Na. Dennis Gondwe, MSALATO

SHULE ya Sekondari ya Wasichana Msalato inamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi za ujenzi wa miundombinu na kuwatengenezea mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia wanafunzi kwa lengo la kukuza viwango vya taaluma nchini.

Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana, Msalato, Mwl. Mwasiti Msokola alipokuwa akiongelea juhudi za serikali katika ujenzi wa miundombinu


Shukrani hizo zilitolewa na Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana, Msalato, Mwl. Mwasiti Msokola alipokuwa akiongelea juhudi za serikali katika ujenzi wa miundombinu mbele ya ugeni kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar uliotembelea shule hiyo.

Tunamshukuru sana Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa upande wa elimu Shule ya Sekondari ya wasichana Msalato ametuona kwa sababu mwaka jana ametuletea fedha shilingi 428,000,000 kutuwezesha kujenga mabweni mawili ya maadalizi ya kupokea wanafunzi wa kidato cha tano. Vilevile, tukapewa vyumba saba vya madarasa na matundu 10 ya vyoo. Haikutosha tukapewa tena shilingi 260,000,000 kwa ajili ya kujenga mabweni mengine mawili. Kukamilika kwa miundombinu hiyo kumepunguza msongamano wa wanafunzi darasani na katika mabweni kila mwanafunzi ana kitanda chake. Tunamshukuru sana rais wetu” alisema Mwl. Msokola kwa sauti ya shukrani.

Wakati huohuo, Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Sekondari Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Zainab Abdallah alisema kuwa motisha kwa walimu imesaidia kuinua hali ya taaluma.Motisha ni kila kitu katika elimu kama hakuna motisha ni kazi ngumu sana. Tarehe 17 Februari, 2024 tulifanya kikao cha wadau wa elimu pamoja na utoaji tuzo kwa walimu waliofanya vizuri katika masomo yao ili tujadiliane jinsi ya kuboresha elimu. Halmashauri tuliipatia shule hii tuzo na tuna utaratibu wa kununua alama ‘A’ kwa kila mwalimu anayezalisha ‘A’ tunailipa shilingi 10,000. Kwa hiyo hapa walinimalizia kibubu changu hapa Msalato. Hapa kulikuwa na mwalimu ana ‘A’ 86 za Kiswahili, mwalimu ana ‘A’ 78 Baiolojia na mwalimu ana ‘A’ 74 za Kemia na wote tuliwazawadia” alisema Mwl. Zainab.

Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Sekondari Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Zainab Abdallah akifuatilia majaribio katika Maabara ya Kemia 


Wakiwa shuleni hapo, timu ya wageni kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar walielezwa usimamiaji wa nidhamu ya walimu na wanafunzi, jitihada za shule kumaliza mada kwa wakati na wanafunzi kufanya majaribio ya sayansi kwa vitendo.





MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma