Tamisemi yajivumia taaluma Bunge Sekondari

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

OFISI ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa inajivunia maendeleo ya kitaaluma katika Shule ya Sekondari ya wasichana Bunge kufuatia uwekezaji waliofanya na serikali shuleni hapo.

Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu Ofisi ya Rais, Tamisemi, Mwl. Ernest Hinju (katikati) akisisitiza jambo


Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu Ofisi ya Rais, Tamisemi, Mwl. Ernest Hinju alipoongoza ujumbe kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kutembelea shule hiyo.

Mwl. Hinju alisema “leo tulikuwa katika ziara ya kuwakaribisha na kuwatembeza wageni wetu kutoka Zanzibar ambao ni Mkurugenzi wa Elimu Maandalizi na Msingi na Mkurugenzi wa Elimu ya Sekondari pamoja na wasaidizi wao. Lengo ni kuja kujifunza kwa pande mbili jinsi wanavyoendesha elimu. Katika shule ya sekondari ya wasichana Bunge pamoja na mambo mengine tumeweza kuongea na wanafunzi na tumewakuta wanafunzi wanapendeza na wanahari ya kujifunza. Shule ya Sekondari ya wasichana Bunge imejengwa kwa hisani ya wabunge wa Tanzania na imethibitika jitihada ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan alivyoweza kuongeza majengo mengine mengi kwa haraka. Leo shule ina wanafunzi wa kidato cha tano na sita; na tumeshuhudia matokeo yanapanda kwa kasi na walimu wanajituma sana. Tumetembelea maabara na wanafunzi wanaweza kuonesha kazi wanazofanya vizuri sana.

Akisoma taarifa ya shule, Mkuu wa Shule hiyo, Mwl. Salome Mkombola alisema kuwa shule yake ina mikakati ya kukuza taaluma. “Mikakati hiyo ni kuzingatia ratiba ya vipindi vyote kufundishwa. Pia tumekuwa na mitihani ya mara kwa mara inayosahihishwa na kufanyiwa tathimini. Mkakati mwingine tumekuwa tukiwatambua na kuwasaidia wanafunzi ambao hawafanyi vizuri kwenye mitihani yao na kuendesha madarasa rekebishi pamoja na kutumia vipindi vya ziada ili kumaliza mihtasari mapema na kupata muda mzuri wa kufanya mapitio ya maeneo ambayo yamekuwa yakiwatatiza wanafunzi” alisema Mwl. Mkombola.

Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Bunge, Mwl. Salome Mkombola akisoma mikakati ya kukuza taaluma


Akiongelea kupanda kwa taaluma, mwalimu wa taaluma msaidizi, Mwl. Stephano Chipuza alisema kuwa taaluma imekuwa ikipanda kila mwaka. “Kidato cha sita awamu ya kwanza tulikuwa na Daraja la kwanza wanafunzi 17, daraja na pili wanafunzi 92 na daraja la tatu wanafunzi 38. Hatukuwa na daraja la nne wala sifuri. GPA ile hatukuridhika nayo. Mwaka jana daraja la kwanza walikuwa wanafunzi 54 maana yake walipanda kutoka wanafunzi 17 mapaka 54. Daraja la pili wanafunzi 86 na daraja la tatu wanafunzi 33. Hivyo, GPA ikawa inasogea kutoka 3.6 mpaka 2.8” alisema Mwl. Chipuza.



Mwl. Stephano Chipuza, Mtaaluma msaidizi


MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma