Dodoma Sec kuongeza ufaulu kula mwaka

 Na. Dennis Gondwe, DODOMA

SHULE ya Sekondari Dodoma imekuwa ikiongeza ufaulu kila mwaka ikifikisha zaidi ya asilimia 97 ya ufaulu wa jumla kutokana na ushirikiano uliopo baina ya wanafunzi, uongozi wa shule na serikali.

Mkuu wa Shule ya Sekondari Dodoma, Mwl. Francis Tumaini alipokuwa akielezea mwenendo wa shule yake katika ufaulu


Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Shule ya Sekondari Dodoma, Mwl. Francis Tumaini alipokuwa akielezea mwenendo wa shule yake kwa wageni kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar waliotembelea shule hiyo kwa lengo la kujifunza.

Mwl. Tumaini alisema “kwa hali ya ufaulu, tunaongeza ufaulu kila mwaka. Kwa mwaka juzi ufaulu kwa daraja la kwanza hadi la tatu, lengo la serikali tufikie asilimia 50. Sisi tulikuwa na asilimia 65. Mwaka jana tukawa na asilimia 67 na mwaka huu tuna asilimia 68. Kwa ufaulu wa jumla kwa mwaka huu tuna asilimia zaidi ya 97. Kwa matokeo ya kidato cha Nne, tulikuwa na wanafunzi 308 tuliowasajili, waliofanya mtihani walikuwa 305. Walipata daraja la kwanza ni 41, daraja la pili 101 na daraja la tatu 64. Hawa ukiwatafuta utakuta tupo asilimia 68 ambao wanaweza kwenda vyuo na sekondari za juu. Hii inatuonesha tunapiga hatua ya kitaaluma kwenda mbele”.

Akiongelea matokeo ya kitaifa ya kidato cha sita kwa mwaka jana alisema kuwa shule yake ilipata daraja la kwanza hadi la tatu pekee. “Hatukuwa na daraja la nne wala sifuri. Ninawashukuru viongozi wetu wote kuanzia Ofisi ya Rais, Tamisemi, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na Ofisi ya Mkurugenzi wa Jiji hadi kwenye ofisi za kata tupo nao kwa karibu sana kuyafikia mafanikio haya” alisema Mwl. Tumaini.

Alisema kuwa shule yake imekuwa ikiwajengea uwezo viongozi wa serikali ya wanafunzi. “Tuna serikali ya wanafunzi ambao tunawafundisha na kuwajenga kuwa viongozi wa imara wa kesho. Kule wanaingia kwenye kamati mbalimbali zote zinaanza na walimu na zinashuka hadi kwa wanafunzi. Lakini pia tuna bustani za mbogamboga kwa ajili ya kuwafundisha wanafunzi umuhimu wa bustani hizo katika lishe bora kwao na kwa jamii inayowazunguka” aliongeza Mwl. Tumaini.





MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma