JAMII DODOMA YASHAURIWA KUSAIDIA WATOTO WENYE MAHITAJI MAALUM

 

Na. Dennis Gondwe, HOMBOLO BWAWANI

JAMII imeshauriwa kutenga muda kuwasaidia watoto wenye mahitaji maalum katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma ili waweze kujimudu na kufikia malengo ambayo taifa linapenda.

Mdau wa elimu katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Tatu Mwangu akimpatia zawadi mtoto


Kauli hiyo ilitolewa na mdau wa elimu katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Tatu Mwangu alipoungana na Jumuiya ya Shule ya Msingi Feza tawi la Dodoma kutoa msaada wa viti mwendo nane na vifaa vya elimu kwa watoto wenye mahitaji maalum katika Shule ya Msingi Hombolo Bwawani.

Mwl. Mwangu alisema “katika hali ya kawaida sisi kama jamii tunawajibika kuwasaidia wote wasio na uhitaji na wenye uhitaji maalum kufikia ndoto zao. Leo kupitia familia ya Shule ya Feza wamepewa vifaa vya kuwasaidia katika kujifunza na kuweza kutembea kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine kwa wale wenye changamoto ya viungo. Tuishukuru familia ya Shule ya Feza kwa kutushirikisha wazazi. Kwa kufanya hivyo kila mwaka tunakusanya kama sadaka kwa ajili ya watoto wenye uhitaji sehemu mbalimbali. Kwa mwaka huu Hombolo Bwawani tumeipa kipaumbele na mpokee hiki tulichokileta kwenu. Tuwashukuru viongozi ngazi ya kata, halmashauri na kitaifa kwa kutambua umuhimu wa elimu kwa watoto wenye mahitaji maalum. Kwa juhudi wanazoendelea kuzitoa kuhakikisha watoto hawa wanakuwa salama na wanafikia yale malengo ambayo tunayatarajia”.

Alisema kuwa watoto hao wana uhitaji wa kusaidiwa. “Kutokana na umuhimu huo tunaona ni thamani kubwa sana tuwapende kama tunavyojipenda sisi, tuwapende watoto wetu hawa na tuwasaidie walimu kwa kushirikiana na wazazi. Kuhakikisha mafanikio ya kitaifa yanafikiwa na mafanikio ya kielimu kwa watoto hawa yanafikiwa” alisema Mwl. Mwangu kwa hisia.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Hombolo Bwawani, Mwl. Pascal Ngoda aliwakaribisha wageni hao na kuwashukuru kwa zawadi.

Aliwataarifu kuwa serikali inatambua haki na usawa kwa watoto wenye mahitaji maalum. “Mpaka sasa tuna watoto wenye mahitaji maalum ya aina tano tofauti. Tuna watoto wenye ulemavu wa viungo, ambao tunashukuru wageni wetu wametuletea viti mwendo kwa ajili ya kuwasaidia kutembea kutoka bwenini hadi shuleni. Lakini pia watoto wenye ulemavu wa ngozi yaani albino, lakini tuna watoto wenye changamoto ya akili. Tuna watoto wenye uono afifu na watoto wasioona kabisa. Msisite kututembelea nyie ni sehemu ya faraja kwetu sisi mnapokuja mara kwa mara hata bila chochote sisi tunawakaribisha na tunawapokea tunatamani na tunajiona sisi ni sehemu ya jamii” alisema Mwl. Ngoda.

Akishukuru kwa niaba ya watoto wenye mahitaji maalum, Dickson Frank alisema kuwa Mungu awabariki wageni hao. “Kwa niaba ya wanafunzi wenzangu napenda niwashukuru wageni wetu mliokuja kututembelea leo Mungu awabariki na awaongezee pale mlipopunguza. Kwenu mnaona ni kidogo lakini kwetu tunaona ni kikubwa sana. Mwenyezi Mungu atembee nanyi awape mkono katika safari yenu. Sisi hatukutarajia tutaletewa kitu kama hiki ila tunashukuru sana Shule ya Feza. Wengine walikuwa hawana viti mwendo sasa tumepata kwa ajili ya kuwatembeza wenzetu” alisema kwa sauti ya shukrani.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma