VYOMBO VYA HABARI JIJI LA DODOMA VYAPONGEZWA KUJALI WENYE MAHITAJI MAALUM

 

Na. Dennis Gondwe, HOMBOLO BWAWANI

VYOMBO vya habari katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma vimepongezwa kwa utayari wao kutangaza mafanikio na changamoto wanazopitia watoto wenye mahitaji maalum katika Shule ya Msingi Hombolo Bwawani.

Diwani wa Kata ya Hombolo Bwawani, Ased Ndajilo akikabidhi zawadi kwa watoto wenye mahitaji maalum

Diwani wa Kata ya Hombolo Bwawani, Ased Ndajilo akihamasisha jamii kuchangia watoto wenye mahitaji maalum


Pongezi hizo zilitolewa na Diwani wa Kata ya Hombolo Bwawani, Ased Ndajilo alipokuwa akitoa shukrani kwa Jumuiya ya Shule ya Msingi Feza tawi la Dodoma walipotembelea Shule ya Msingi Hombolo Bwawani kutoa zawadi ya viti mwendo nane na vifaa vya elimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu wa Shule ya Msingi Hombolo Bwawani.

Ndajilo alisema “napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mheshimiwa Rais, mama yetu Samia Suluhu Hassan, Mbunge na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde kwa kazi nzuri wanayofanya katika Kata ya Hombolo Bwawani. Sina budi kushukuru Shule ya Msingi Feza kwa kutuletea msaada wa viti mwendo nane na vifaa vitakavyowasaidia watoto kwenye mwendo na kwenye masomo yao, kama mnavyowaona wengine kunyanyuka ni shida. Hii ni faraja sana kwetu Halmashauri ya Jiji la Dodoma, tunapenda kutoa pongezi na shukurani kwa Shule ya Msingi Feza”.

Aidha, alivishukuru vyombo vyote vya habari ambavyo vimekuwa vikitangaza mafanikio na changamoto za shule hiyo na kuwavuta wanajamii kutoa msaada. “Nisisitize pia kwa yeyote anayewiwa akiwa na uwezo na nguvu, hawa ni watu wanaohitaji mahitaji ya faraja, fedha, nguo na afya na mambo mengine ambayo mtu ataguswa nayo. Kwa hiyo mimi mwenye kata nina wakaribisha wote wenye kuguswa wanaweza kuja na kuchangia kadri wanavyo weza” alisisitiza Ndajilo.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Hombolo Bwawani, Mwl. Pascal Ngoda aliwakaribisha wageni hao na kuwashukuru kwa zawadi.

Aliwataarifu kuwa serikali inatambua haki na usawa kwa watoto wenye mahitaji maalum. “Mpaka sasa tuna watoto wenye mahitaji maalum ya aina tano tofauti. Tuna watoto wenye ulemavu wa viungo, ambao tunashukuru wageni wetu wametuletea viti mwendo kwa ajili ya kuwasaidia kutembea kutoka bwenini hadi shuleni. Lakini pia watoto wenye ulemavu wa ngozi yaani albino, lakini tuna watoto wenye changamoto ya akili. Tuna watoto wenye uono afifu na watoto wasioona kabisa. Msisite kututembelea nyie ni sehemu ya faraja kwetu sisi mnapokuja mara kwa mara hata bila chochote sisi tunawakaribisha na tunawapokea tunatamani na tunajiona sisi ni sehemu ya jamii” alisema Mwl. Ngoda.

Akishukuru kwa niaba ya watoto wenye mahitaji maalum, Dickson Frank alisema kuwa Mungu awabariki wageni hao. “Kwa niaba ya wanafunzi wenzangu napenda niwashukuru wageni wetu mliokuja kututembelea leo Mungu awabariki na awaongezee pale mlipopunguza. Kwenu mnaona ni kidogo lakini kwetu tunaona ni kikubwa sana. Mwenyezi Mungu atembee nanyi awape mkono katika safari yenu. Sisi hatukutarajia tutaletewa kitu kama hiki ila tunashukuru sana Shule ya Feza. Wengine walikuwa hawana viti mwendo sasa tumepata kwa ajili ya kuwatembeza wenzetu” alisema kwa sauti ya shukrani.

Jumuiya ya Shule ya Msingi Feza tawi la Dodoma ilifanya Charity Marathon na kukusanya fedha na kuchangia viti mwendo nane na vifaa vingine vya elimu kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum wa Shule ya Msingi Hombolo Bwawani jijini Dodoma.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo