JIJI LA DODOMA LAMSHUKURU DKT. SAMIA KUJALI WATOTO WENYE MAHITAJI

 

Na. Dennis Gondwe, HOMBOLO BWAWANI

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali watoto wenye mahitaji maalum.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Issa Kambi (kushoto) akimsaidia mtoto mwenye mahitaji maalum kutembea. Kulia ni Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Feza Dodoma, Yunus Khusanbaev nae akimsaidia mtoto kutembea


Shukrani hizo zilitolewa na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Issa Kambi katika hafla ya kupokea viti mwendo na vifaa vya shule kwa watoto wenye mahitaji maalum katika Shule ya Msingi Hombolo Bwawani iliyopo jijini Dodoma.

Mwl. Kambi alisema “tunamshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kwa watoto hawa wenye mahitaji maalum katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Mfano, katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma Mheshimiwa Rais kupitia Ofisi ya Rais, Tamisemi anatuletea shilingi 26,000,000 kila mwezi kwa ajili ya chakula cha watoto hawa. Tunapopata wadau kuja kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais tunafurahi sana. Kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, John Kayombo aliyeniagiza niwashukuru kwa kutusaidia. Na yeye kwa mwaka huu ametenga shilingi 20,000,000 kwa ajili ya vifaa vya watoto hawa wenye mahitaji maalum katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma”.

Akiongelea msaada wa vifaa vilivyotolewa na Shule ya Msingi Feza, alisema kuwa halmashauri imekuwa ikipokea vifaa kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum kila mwaka. “Na msimu huu wamefanya jambo kubwa zaidi kutuletea viti mwendo nane kwa watoto wetu hawa ambao baadhi viti vyao vilikuwa vimechakaa na wengine walikuwa hawana kabisa. Hili ni jambo zuri na kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan” alisema Mwl. Kambi.

Mwl. Kambi alisema kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ina vituo 10 vyenye watoto watoto wenye mahitaji maalum. “Nimshukuru pia Diwani wa Kata ya Hombolo Bwawani ambae tupo nae hapa kwa kazi nzuri anayoifanya kuendelea kuwalea hawa watoto na kusaidia kwenye ujenzi wa miundombinu. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Diwani” alisema Mwl. Kambi.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Hombolo Bwawani, Mwl. Pascal Ngoda aliwakaribisha wageni hao na kuwashukuru kwa zawadi.

Aliwataarifu kuwa serikali inatambua haki na usawa kwa watoto wenye mahitaji maalum. “Mpaka sasa tuna watoto wenye mahitaji maalum ya aina tano tofauti. Tuna watoto wenye ulemavu wa viungo, ambao tunashukuru wageni wetu wametuletea viti mwendo kwa ajili ya kuwasaidia kutembea kutoka bwenini hadi shuleni. Lakini pia watoto wenye ulemavu wa ngozi yaani albino, lakini tuna watoto wenye changamoto ya akili. Tuna watoto wenye uono afifu na watoto wasioona kabisa. Msisite kututembelea nyie ni sehemu ya faraja kwetu sisi mnapokuja mara kwa mara hata bila chochote sisi tunawakaribisha na tunawapokea tunatamani na tunajiona sisi ni sehemu ya jamii” alisema Mwl. Ngoda.

Akishukuru kwa niaba ya watoto wenye mahitaji maalum, Dickson Frank alisema kuwa Mungu awabariki wageni hao. “Kwa niaba ya wanafunzi wenzangu napenda niwashukuru wageni wetu mliokuja kututembelea leo Mungu awabariki na awaongezee pale mlipopunguza. Kwenu mnaona ni kidogo lakini kwetu tunaona ni kikubwa sana. Mwenyezi Mungu atembee nanyi awape mkono katika safari yenu. Sisi hatukutarajia tutaletewa kitu kama hiki ila tunashukuru sana Shule ya Feza. Wengine walikuwa hawana viti mwendo sasa tumepata kwa ajili ya kuwatembeza wenzetu” alisema kwa sauti ya shukrani.

Ikumbukwe kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ina watoto wenye mahitaji maalum 1,050 na Shule ya Msingi Hombolo Bwawani ikiwa na watoto 44 wenye mahitaji maalum.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma