JIJI LA DODOMA LAZINDUA ZOEZI LA UBAINISHAJI WATOTO WENYE MAHITAJI MAALUM

Na. Dennis Gondwe, HOMBOLO BWAWANI

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imezindua zoezi la ubainishaji watoto wenye mahitaji maalum katika jamii ili waweze kupata haki yao ya elimu na matunzo kwa mujibu wa sheria.





Kauli hiyo ilitolewa na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Issa Kambi alipokuwa akizindua zoezi la ubainishaji watoto wenye mahitaji maalum katika jamii uzinduzi uliofanyika katika Shule ya Msingi Hombolo Bwawani iliyopo Kata ya hombolo Bwawani jijini Dodoma.

Kambi ambae ni Afisa Elimu Maalum katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma alisema “kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ambae alipenda sana kuwa nasi hapa leo napenda kuzindua rasmi zoezi la ubainishaji watoto wenye mahitaji maalum kwa maana ya kwenda kuwatafuta mtaani na kuwaleta kwenye vituo vyetu kama hiki na vitengo vingine. Zoezi litafanyika katika mitaa nane ya Itega, Salama, Lugala, Mnyakongo, Mtube, Nala, Chigongwe na Mbalawala”.

Alisema kuwa lengo la zoezi hilo ni kuwabaini watoto hao mahali walipo na kuwasogeza kwenye huduma na kuwapatia afua stahiki ikiwa ni pamoja na elimu na matunzo. “Tunafahamu kwamba baadhi ya familia zinaamini watoto hawa hawawezi kufanya mambo, lakini tunapokwenda kufanya ubainishaji tunawatia moyo na kuwashawishi kuwaleta watoto hawa shule. Kuanzia ngazi za familia tunapeleka elimu na baadae tunawaleta kwenye vituo kama hivi na kama mlivyoona watoto hawa wanafuraha” alisema Kambi.

Akiongelea umuhimu wa zoezi hilo, Mkazi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma Juliana Linus alisema kuwa zoezi hilo ni muhimu kwa sababu linakwenda kuwapatia haki ya msingi watoto wenye mahitaji maalum katika Jiji la Dodoma. “Ni kweli wapo baadhi ya wazazi ambao wamekuwa na tabia ya kuwaficha watoto wao wenye ulemavu jambo linalowanyika haki watoto hao kupata elimu, afya na malezi bora” alisema Linus.

Zoezi la uzinduzi wa ubainishaji watoto wenye mahitaji maalumu katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma lilihudhuriwa na Jumuiya ya Shule ya Msingi Hombolo Bwawani ambayo ni shule jumuishi, Diwani wa Kata ya Hombolo Bwawani, maafisa waandamizi kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma na wawakilishi wa Jumuiya ya Shule ya Msingi Feza tawi la Dodoma na wawakilishi wa serikali ya mtaa.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma