Teknolojia Bunifu ya Mifugo yasogezwa maonesho ya Nanenane

Na. Husna Rajabu, DODOMA

Taasisi ya Wakala wa vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (LITA) imeteka umakini wa wageni katika maonesho ya Nanenane jijini Dodoma kwa kuonesha teknolojia bunifu zinazolenga kuongeza thamani ya mazao ya mifugo na kuboresha maisha ya wafugaji.




Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Idara ya Utafiti na Huduma za Ushauri (LITA), Joseph Msemwa, alisema kuwa taasisi hiyo imeweka bayana bidhaa na huduma kadhaa ambazo ni matokeo ya kazi za vijana wa kitanzania.

Alisema kuwa maonesho ya Nanenane ni sehemu muhimu ya kuonesha bidhaa na teknolojia zitakazobadilisha taswira ya uchumi wa wananchi. “Tupo hapa kwenye maonesho ya Nanenane jijini Dodoma, tumeleta teknolojia mbalimbali zinazohusiana na bidhaa za maziwa. Pia tuna teknolojia ya uchakataji wa ngozi ambapo tunawafundisha vijana wetu namna ya kuchakata ngozi, kuanzia ikiwa mbichi mpaka ifike hatua ya mwisho ya utengenezaji wa bidhaa. Kama mnavyojionea bidhaa za ngozi zipo za aina tofauti tofauti ikiwemo viatu, hereni na mikanda” alisema Msemwa.

Pia alieleza kuhusu teknolojia ya maziwa wanayofundisha kuwa ina faida kubwa kwa wafanyabaishara na wajasiriamali. “Tunachakata maziwa na kuongeza thamani yake, tunatengeneza maziwa mtindi, mtindi yogati na siagi. Tunatoa mafunzo ya kufanya shughuli hiyo kwa vijana wetu ili wapate ujuzi na kujitegemea kiuchumi” alisema.

Moja ya kivutio kikubwa ni mashine ya kutotolesha vifaranga iliyobuniwa na vijana wa taasisi ya (LITA) wakiwa chuoni na inapatikana kwenye maonesho ikitarajiwa kusaidia wafugaji wadogo na wakubwa.

Aidha, (LITA) imeleta teknolojia ya mfumo wa uchakataji wa mbolea inayotokana na mifugo kama ng'ombe, mbuzi au kuku kwa lengo la kuzalisha nishati. “Teknolojia hii inaitwa ‘biogas’. Ni teknolojia inayobebeka, unaweza kuhamisha kutoka sehemu moja kwenda nyingine, na inaweza kutumika mashambani na kwenye matumizi ya nyumbani” alieleza Msemwa.

Nae, Mkufunzi wa Chuo cha Mifugo, Joyce Balabala alizungumzia kuhusiana na ufugaji wa sungura. “Vijana wetu tunawaelekeza namna ya ufugaji sahihi wa sungura na jinsi ambavyo sungura wanaweza kuzalisha vitu mbalimbali. Kwa mfano kupitia sungura unaweza kupata nyama iliyo nzuri na bora lakini pia tumegundua mkojo wa sungura unatumika kwaajili ya mbolea” alisema Balabala.

Aidha, aliishukuru Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa maandalizi ya maonesho ya Nanenane. “Maandalizi ya mwaka huu ni mazuri zaidi, nimejaribu kuangalia kwenye mabanda mengine nimeona watu ni wengi na maandalizi ni ya hali ya juu.

MWISHO

Imehaririwa na Nancy Kivuyo

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo