TAKUKURU yapewa rai kuboresha mikakati ya kutokomeza rushwa

Na. Nancy Kivuyo, DODOMA

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) imeeleza kuwa katika kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Tanzania imejipanga kutoa elimu na kusisitiza wananchi kuepuka kupokea rushwa kwaajili ya kuchagua viongozi.



Hayo yalielezwa na Mratibu wa Banda la TAKUKURU, Suzana Raymond wakati akizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma aliyetembelea banda hilo katika maonesho ya wakulima Nanenane yanayoendelea Nzuguni jijini Dodoma.

Alisema kuwa banda la TAKUKURU limejikita katika kutoa elimu na kupokea taarifa zinazohusu masuala ya rushwa. Pamoja na majukumu yote, wakati mwingine tunapokea ushauri mbalimbali kwasababu sisi tunaweza tusione tunachokifanya lakini walio nje ndio wanaona nini tunakifanya na huwa tunapeleka ngazi za juu na wao wanazifanyia kazi kwa kadri inavyotakikana” alisema Raymond.

Alisema kuwa lengo la kuwepo katika maonesho ya Nanenane ni kuhakikisha wanatoa elimu ya kutosha kwa jamii hasa kuelekea uchaguzi mkuu. “Lakini katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu tunatumia fursa hii kuwaelimisha wananchi juu ya athari za kuchagua viongozi baada ya kupokea rushwa. Kupitia maonesho haya tuna uelimishaji wa nje ambao wenzetu wapo wanazunguka sehemu mbalimbali huko nje ili kuendelea kutoa elimu na kuhakikisha suala la rushwa linatokomezwa” alimalizia Raymond.



Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj. Jabir Shekimweri alianza kwa kuipongeza TAKUKURU kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuhakikisha mapambano ya kutokomeza rushwa yanafanikiwa. “Rushwa ipo kwenye historia ya dunia, lakini ninyi mnapaswa kuendelea na mapambano na kuhakikisha rushwa inatokomezwa kwa kubadilisha mbinu za ufanyaji kazi. Mapambano hayo yasiishie kwenye watu wazima walio makazini tu bali mbinu nyingine mbadala zitumike ili kuhakikisha suala hili linabaki historia” alisema Alhaj. Shekimweri.

Alimalizia kwa kutoa rai kwa TAKUKURU kuhakikisha wanabadilisha mbinu na mazingira ya ufanyaji kazi. “Jambo la kwanza, nashauri kuwa ni muhimu kuhakikisha rika dogo wanapewa elimu ya kutosha ili wakue na mkakati huo utakaowajengea mzizi wa uzalendo mapema. Jambo la pili kuhakikisha kuwa rika la utegemezi ambalo baada ya muda wanaingia kwenye mazingira ya elimu ya juu na ajira wanajengewa uwezo wa nidhamu katika fedha, katika kujitegemea na kuwajibika ili wanapoingia kazini suala la rushwa lisiwe tatizo tena. Kwenye uchaguzi tunawategemea sana kuwa mtafanya vizuri zaidi ili kuepusha makovu yatakayoachwa baada ya uchaguzi” alimaliza Alhaj. Shekimweri.

Maonesho ya Nanenane kitaifa yapo katika siku yake ya sita katika viwanja vya Nanenane, Nzuguni yakiongozwa na kaulimbiu isemayo “Chagua viongozi bora kwa maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi”

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo