DC Shekimweri ashauri TMDA kuwa wabunifu

Na. Leah Mabalwe, DODOMA

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj. Jabir Shekimweri, ameitaka Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kuwa wabunifu na kutumia teknolojia ya kisasa katika shughuli zake za ukaguzi wa dawa na vifaa tiba nchini, ili kuongeza ufanisi na kuimarisha usalama wa wananchi.



Alisema hayo wakati alipotembelea banda la TMDA katika Maonesho ya Wakulima Nanenane yanayofanyika katika viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.

Alisema kuwa anawapongeza kwa kuendelea kutoa huduma ikiwemo kusajili, kudhibiti na kufuatilia ubora wa dawa. “Nawapongeza kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kulinda afya za wananchi kupitia udhibiti wa dawa na vifaa tiba. Hata hivyo, katika dunia ya sasa ya teknolojia, mnapaswa kuwa wabunifu zaidi katika mbinu zenu za ukaguzi ili kuweza kufika maeneo mengi kwa haraka na kwa ufanisi zaidi na kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu matumizi sahihi ya dawa” alisema Alhaj. Shekimweri.

Pia aliongezea kwa kuwasisitiza kuendelea kushirikiana kwa karibu na vyombo vingine vya serikali. “Na niwaase tu Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba kuendelea kushirikiana na baadhi ya taasisi nyingine ili kuwafikia wananchi sehemu mbalimbali kwaajili ya kutoa elimu kuhusu matumizi ya dawa na kuhakikisha kwamba bidhaa zote za afya zinazotumika nchini ni salama na zenye ubora unaotakiwa” aliongeza Alhaj. Shekimweri.

Kwa upande wake Mkaguzi wa Dawa Mwandamizi, Benedict Brashi alimshukuru Mkuu wa Wilaya ya Dodoma kwa kutembelea banda lao na kuahidi kufanyia kazi yale ambayo wameshauriwa. “Mamlaka hii inaendelea kuboresha mifumo yake ya udhibiti na inaendelea kuwekeza kwenye teknolojia za kisasa pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wake kwa lengo la kutoa huduma bora zaidi kwa watanzania” alisema Brashi.

Maonesho ya Nanenane kitaifa yapo katika siku yake ya sita katika viwanja vya Nanenane, Nzuguni yakiongozwa na kaulimbiu isemayo “Chagua viongozi bora kwa maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi”

MWISHO

Imehaririwa na Nancy Kivuyo

 

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo