Sura mpya ya kilimo cha vitunguu yaonesha mafanikio

Na. Husna Rajabu, DODOMA

Kitunguu kimekuwa ni miongoni mwa zao la biashara chenye faida kubwa na hulimwa karibu maeneo yote nchini hasa maeneo ya miinuko ya kaskazini mwa Tanzania.



Katika maonesho ya wakulima Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma vipando bustani vya Halmashauri ya Jiji la Dodoma vimejumuisha teknolojia ya ulimaji vitunguu kwa njia ya asili katika eneo dogo na kupata mazao mengi.

Afisa Kilimo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Madei Kidai alieleza mchakato wa kilimo hicho chenye tija kibiashara. “Ili kufanikisha kilimo cha vitunguu, ni lazima uanze na maandalizi ya shamba. Pia, tunawahimiza wakulima kutafuta mbegu bora, kuandaa matuta vizuri, na kuhamisha miche kutoka kwenye kitalu baada ya muda muafaka. Hapa kwetu tumetumia mbinu hizi, na matokeo yanaonekana kama hivi mnavyoona” alieleza Kidai.

Kwa mujibu wa Kidai, baada ya kupanda, hatua muhimu zinazofuata ni umwagiliaji na udhibiti wa wadudu na magonjwa. Alisisitiza kuwa wametumia viwatilifu vinavyosaidia kudhibiti wadudu kama vidudu mafuta na viducali na magonjwa kama fangasi ambayo kwa kawaida hushambulia vitunguu.

Kwa upande mwingine, Afisa Kilimo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Nkunde Kimweri alieleza mbinu za kilimo hai ‘organic’ walizotumia. “Hapa katika shamba letu la mfano, tulianza kwa kuandaa matuta na kuchanganya mbolea ya samadi. Kwa kila tuta tulitumia ndoo tatu za mbolea ya samadi, baada ya kuchanganya mbolea na udongo, tulimwagilia maji na kuacha ardhi ipoe kwa siku mbili kabla ya kupanda vitunguu” alisema Kimweri.

Alimalizia kusema kuwa mbegu wanazichagua kwa umakini mkubwa sana kwenye maduka ya pembejeo za kilimo. “Mbegu yetu, inaitwa Red Planet F1, tuliipanda tarehe 20 Mei, 2025. Muhimu zaidi ni kwamba kilimo hiki chote tumetumia mbolea na dawa za asili kama mnavyoona matokeo ni mazuri na vitunguu vimestawi vizuri. Alimaliza Kimweri.

Vitunguu ni zao la kibiashara lenye tija kubwa na linafanya vizuri mkoani Dodoma, linapaswa kupewa kipaumbele na wakulima wengi kwa lengo la kukuza biashara ya vitunguu na kuongeza pato la uchumi wa mkoa na wananchi wote kwa ujumla.




MWISHO

Imehaririwa na Nancy Kivuyo 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo