Waziri Mchengerwa atoa Maagizo mahususi kwa Wakuu wa Mikoa na Wakurugenzi

OR. TAMISEMI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Tamisemi, Mohamed Mchengerwa amewaelekeza wakuu wa mikoa kuwasimiamia Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuzingatia vipaumbele vya mwaka 2025/26 kikamilifu.




Waziri Mchengerwa alitoa maelekezo hayo wakati akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya wizara na taasisi zake kwa mwaka 2025/26.

Alisema kuwa vipaumbele vya kuzingatia ni kuhakikisha ukusanyaji wa mapato unafikia malengo na kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya afya ya msingi, elimu ya msingi na sekondari kulingana na mipango iliyowekwa.

Aidha, aliwataka kusimamia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidigitali ikiwemo uwekaji na matumizi ya mifumo na miundombinu ya TEHAMA katika mikoa na mamlaka za serikali za mitaa ikiwa ni pamoja na vituo vya huduma za afya na elimu.

Vilevile, aliwaagiza kuhakikisha mapato katika mikoa na mamlaka za serikali za mitaa yanakusanywa kupitia mifumo ya TEHAMA ya serikali pamoja na kufanya ufuatiliaji wa karibu wa mifumo hiyo ili kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato.

Alisema kuwa mikoa na mamlaka za serikali za mitaa zihakikishe zinatekeleza Mikakati ya Uchumi wa Buluu, nishati safi ya kupikia na mabadiliko ya tabia nchi na utunzaji wa mazingira.

Vilevile, aliagiza mikoa na mamlaka za serikali za mitaa kuendelea kuimarisha mifumo stahimilivu na endelevu ya utoaji wa huduma bora za afya, ustawi wa jamii na lishe ili kuboresha huduma ambayo ni nguzo muhimu katika kufanikisha utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa wote.

Pia, aliwataka wakuu wa mikoa na wakurugenzi kuhakikisha watoto walio chini ya miaka mitano wanajiunga kwenye vituo vya jamii vya kulelea watoto wadogo mchana. “Kila halmashauri itapimwa utekelezaji wa vipaumbele hivi kwa kuzingatia miradi iliyotengewa bajeti kwa Mwaka 2025/26” alisisitiza Mchengerwa.

 

Chanzo: www.tamisemi.go.tz

Comments

Popular Posts

Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini ni nyenzo ya utendaji kazi serikalini – Dkt. Biteko

Waziri Mkuu Mgeni Rasmi NBC Dodoma Marathon 2023

Dodoma Sec kuongeza ufaulu kula mwaka