Ujenzi Shule za Sekondari za ziada Suluhu Changamoto ya Umbali

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Kata 41 za Halmashauri ya Jiji la Dodoma zinatarajiwa kunufaika na ujenzi wa shule za sekondari za ziada kwa ajili ya kuhakikisha mtoto anapata elimu katika mazingira mazuri na kutatua changamoto ya umbali wa kupata huduma ya elimu.



Hayo yalisemwa na Mbunge wa Dodoma Mjini, Anthony Mavunde, alipokuwa akitoa hotuba kwa madiwani, wakuu wa divisheni na vitengo, walimu, watendaji wa kata na wanafunzi waliohudhuria katika hafla ya Ugawaji Kompyuta na Printa kwa Shule za Sekondari na maafisa watendaji wa kata jijini Dodoma.

Mbunge wa Jimbo la Dodoma, Anthony Mavunde alisema “moja kati ya mipango yangu mikubwa nayoendelea nayo ni kuendelea kuhakikisha kata zote za Dodoma zina sekondari, tukimaliza hayo tuongeze sekondari za ziada hasa zile ambazo watoto wanatembea umbali mrefu. Mheshimiwa mkuu wa wilaya ukienda pembezoni mwa Jiji la Dodoma, kuna maeneo ambayo watoto walikuwa wanatembea mpaka kilomita 16 kufuata shule. Ukienda Kata ya Chahwa eneo la Mahoma Makulu watoto walikuwa wanatembea umbali mrefu kwenda Ipala Sekondari”.

Kwa upande wake Mkuu wa Shule ya Sekondari Anthony Mavunde, Mwl. Emmanuel Magumba, alimshukuru Mbunge wa Dodoma Mjini kwa ugawaji wa Printa na Kompyuta kwasababu itaenda kutatua changamoto waliyokuwa wanaipata awali katika uandaaji wa mitihani.

“Zoezi hili la ugawaji Kompyuta na Printa nimelipokea kwa mikono miwili na linakwenda kuongeza hali ya utoaji wa mitihani shuleni kwetu kwasababu tulikuwa hatuna vifaa kwa ajili ya kuandalia mitihani na uchapishaji. Hili linakwenda kusaidia wanafunzi wetu kupata elimu bora hasa katika upataji wa mitihani, utoaji wa notisi pamoja na vifaa ambavyo vimewekwa humu kwa ajili ya kusaidia watoto” alisema Mwl. Magumba.



Nae, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Umonga, Angelina Masikini alimshukuru Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini kwa ujio wake na kugawa kompyuta na printa kwa shule zilizopo jijini Dodoma. “Tunamshukuru Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini, Anthony Mavunde kwa kufanya Hafla hii ya Ugawaji wa Kompyuta na Printa kwa Shule za Sekondari jijini Dodoma, tunaamini vifaa hivi vitaenda kuongeza ujuzi wetu darasani na kutupa uwezo mkubwa wa kuendena na mabadiliko ya kiteknolojia yanayoendelea hivi sasa” alishukuru Masikini.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma