Mkutano Mkuu wa 39 wa ALAT wafanyika Dodoma

Na. Aisha Ibrahim, DODOMA

Mkutano mkuu wa 39 wa Mwaka wa Mamlaka ya Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) umefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete Convention Center jijini Dodoma, uliofunguliwa na mgeni rasmi ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kujadili na kufanya tathmini ya mipango ya ALAT na mambo mbalimbali yanayoendelea katika serikali za mitaa.



Akitoa taarifa wakati wa mkutano huo, Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Murshid Ngeze, alisema kuwa katika mkutano wa mwaka huo wamejitahidi kualika viongozi mbalimbali wakiwemo wenyeviti wa mitaa ili kupata maarifa mbalimbali yanayohusiana na uendeshaji wa serikali za mitaa. Hivyo, kwenda kuwa viongozi bora katika mitaa yao. “Mkutano huu tunafanya kila mwaka, lakini mwaka huu tumeenda mbali zaidi kwa kuwaalika wenyeviti wa serikali za mitaa ili watakapofika hapa waweze kupata ujumbe wa moja kwa moja na kujifunza namna ya uendeshaji na utekelezaji wa shughuli zote zinazohusiana na serikali za mitaa” alisema Ngeze.

Katika hatua nyingine, aliishukuru Benki ya NMB kwa kuwa mdau mkubwa wa ALAT na kujitoa katika kuhakikisha shughuli za serikali za mitaa zinazidi kusonga mbele na kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutekeleza miradi mbalimbali nchini. “Tunaishukuru sana Benki ya NMB kwa kuwa mdau wetu mkubwa na kwa mwaka huu ametuunga sana mkono na ifikapo tarehe 13 Machi, 2025 wajumbe wote wa mkutano huu tutakuwa tunasafiri na SGR kutoka Dodoma kwenda Dar es Salaam kwa ufadhiri wa NMB” alishukuru.

Aidha, aliongeza kuwa ALAT imeimalika na kuwa bora kuliko miaka iliyopita kwasababu taarifa za ukaguzi zinawasilishwa mbele ya hadhara na kutolewa ufafanuzi unaojitosheleza. “Mheshimiwa Rais, kwa sasa ALAT imeimarika, mikutano iliyopita taarifa za ukaguzi zilikuwa haziwasilishwi, lakini hivi sasa taarifa hizi zinakuwa wazi na kuwasilishwa vizuri sana” aliongeza Ngeze.

Sambamba na hayo, alifafanua kuwa wamejitahidi kufuata maelekezo ya Rais. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha ushirikiano mzuri kati ya viongozi wa ALAT na taasisi mbalimbali duniani kote. “Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwanza ulisema tuimarishe ushirikiano wa ALAT na taasisi nyingine ikiwemo; Umoja wa Serikali za Mitaa Afrika Mashariki na duniani kote. Hivyo, nikuthibitishie kwamba kauli yako tumeitekeleza kama unavyoona hapa wapo viongozi wa ALAT kutoka Zanzibar na Afrika Mashariki” alifafanua.

Pia alieleza kuwa wamejitahidi kuimarisha ukusanyaji wa mapato kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa. “Hapo nyuma tulikusanya kiasi cha shilingi bilioni 848 kwa mwaka wa fedha 2024/2025 ikiwa ni sawa na asilimia 60 ndani ya halmashauri zetu nchini, na hii yote ni kutekeleza maelekezo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan” alieleza Ngeze.

Alimaliza kwa kusema kuwa “tunafanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya ALAT, na hivi sasa tumeenda mbali zaidi kupitia mkutano huu tunakwenda kuhuisha sheria ya uanzishaji wa ALAT na iendelee kuimarika chini ya ushirikiano mkubwa kuhakikisha maendeleo ya wananchi yanatekelezeka” alisema Ngeze.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma