Dkt. Sagamiko asema, ugawaji jimbo hauna athari kwa huduma zinazotolewa na Jiji la Dodoma

Na, Nancy Kivuyo, DODOMA

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alitoa hofu Baraza la Madiwani kuwa kukidhi vigezo vya ugawaji wa Jimbo la Dodoma Mjini hauna athari katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika kuwahudumia wananchi.



Aliyasema hayo wakati akijibu hoja za madiwani waliohudhuria katika Mkutano maalum wa Baraza la Madiwani kwa ajili ya kupokea taarifa ya mapendekezo ya mgawanyo wa Jimbo la Dodoma Mjini uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri.

“Mgawanyo wa jimbo kwa upande wa tarafa hauna kikwazo chochote, kama ni kata ni kikwazo kwasababu kata moja haiwezi kuwa katika majimbo mawili. Leo tutaangalia zaidi kwenye kata” alisema Dkt. Sagamiko.

Aliongeza kuwa, athari za mgawanyo wa jimbo kimapato unalenga mgawanyo wa majimbo na sio shughuli za kiutendaji. “Niwatoe wasiwasi, utoaji wa huduma kwa wananchi utaendelea kama ilivyokua awali na Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Baraza litakua moja bila kujali jimbo analotoka diwani. Mipango itapangwa kulingana na Halmashauri ya Jiji la Dodoma” alimalizia Dkt. Sagamiko.

Nae, Diwani wa Kata ya Ihumwa, Edward Magawa, aliishukuru serikali kwa kuleta mapendekezo ya mgawanyo wa Jimbo la Dodoma Mjini kwakuwa jiografia yake imekua kubwa na namna ya kuhudumia kata 41 kwa pamoja ni changamoto. “Binafsi niipongeze serikali kwa namna wameona ni vema kugawanya jimbo ili kupata urahisi wa kuhudumia wananchi. Nimpongeze pia Mheshimiwa mbunge kwa kazi nzuri, amejitahidi kuhudumia kata 41 kwa namna alivyoweza lakini sasa itakua rahisi mbunge kuwafikia wananchi na kutatua changamoto kwa urahisi” alisema Magawa.



Kwa upande mwingine, Diwani wa Viti Maalum, Wendo Kutusha alisema “taarifa hii nimeipokea kwa furaha kubwa sana kwasababu kata 41 alizokua anashughulika nazo mbunge wetu Mavunde ni nyingi mno. Kuna majimbo mengine yana kata chache sana. Kwahiyo, ujio wa mgawanyo huu utasaidia mbunge kuzifikia kata zote. Naishukuru sana Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuliona jimbo hili linafaa kuwa na wawakilishi wawili watakaoendeleza maendeleo ya Jiji la Dodoma. Matarajio yangu ni kwamba tunatarajia kuwa shughuli za maendeleo ziwe nyingi na maendeleo yakaonekane katika jamii zetu” alimalizia Kutusha.

Mapendekezo ya kugawanya Jimbo la Dodoma Mjini lenye jumla ya wapiga kura 795,000 na kuwa majimbo mawili, Jimbo la Dodoma Mjini lenye jumla ya watu 412,000 na kata 21 na Jimbo la Mtumba lenye jumla ya watu 383,000 na kata 20 kwa lengo la kusigeza huduma kwa wananchi ambao ndio msingi wa demokrasia ya uwakilishi ndani ya Wilaya ya Dodoma yamepokelewa na kupitishwa kwa kauli moja.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma