Kilimo cha Zabibu ni ajira kwa vijana kujikwamua kiuchumi

Na. Nancy Kivuyo,  MATUMBULU

Vijana wa Kata ya Matumbulu wameendelea kunufaika na fursa za mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kuweza kujikwamua kiuchumi.

 


Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Kikundi cha Kaunda kinachojishughulisha na kilimo cha zabibu, Isack Benjamin alipokuwa akiongea na waandishi wa habari waliofanya media tour kufuatilia wanufaika wa mikopo hiyo katika kata ya matumbulu.

 

Benjamin alisema kuwa mikopo ya asilimia nne inayotolewa na  halmashauri imekua mkombozi kwa vijana wanaopenda kujishughulisha na kuingiza kipato ili kuboresha maisha yao. “Kikundi chetu kilipata mkopo wa shilingi milioni 20, ambapo tupo vijana watano. Tuliwekeza kwenye kilimo cha zabibu kwasababu tuna maeneo makubwa huku na kilimo cha zabibu kinakubali sana. Kiukweli, faida tuliiona, tunasomesha watoto, tunapata mahitaji muhimu na kubwa zaidi tumeweza kuongeza tena ekari tano ambazo kama mnavyoona tunalima tena zabibu” alisema Benjamin.

Nae Afisa Kilimo Kata ya Matumbulu, Aneth Mnana   alisema kuwa kata hiyo ina ardhi nzuri kwa ajili ya kilimo. “Kata ina maji ya kumwagilia mboga mboga na mazao mengine ya muda mfupi. Hawa wakulima tunawapa elimu ya kutosha ili kufanya kilimo chenye tija. Ndio maana mnaona kwasasa wanatoa mazao mazuri sana. Nashauri wataalam wenzangu kuendelea kuwahudumia wananchi kwa weledi ili kilimo kiwe na tija kwa jamii zote kwa siku za usoni” alisema Mnana.

 

Kwa upande wake mkulima Mussa Mlilima aliishukuru serikali kwa elimu ya kilimo kutoka kwa wataalam ambao wameletwa katika Kata ya Matumbulu na kuahidi kuendelea kufanya kilimo chenye tija ili kupata mazao bora. “Namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza watumishi wa kila kada mpaka kwenye kata zetu. Namshukuru pia Mbunge wetu, Anthony Mavunde na Diwani, Emmanuel Chibago kwa jitihada zao katika kuhakikisha kata yetu inakua sehemu ya kilimo bora kwa zabibu na mazao mengine” alisema Mlilima.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

RC Senyamule azipongeza Club za Jogging Dodoma

Usafi wa Mazingira Kipaumbele Kata ya Chamwino