Wananchi washuhudia utiaji saini mkataba wa mradi wa TACTIC

Na. Coletha Charles, DODOMA

Wananchi wa Jiji la Dodoma wamejitokeza kwa wingi kushuhudia hafla ya utiaji saini mkataba wa Mradi wa “Tanzania Cities Transforming Infrastructure and Competitiveness” (TACTIC), unaolenga kuboresha na kujenga miundombinu muhimu katika jiji hilo ikiwa ni pamoja na Uboreshaji wa Ujenzi wa Soko, Vituo vya daladala pamoja na vivuko.




Hafla hiyo, iliyofanyika katika viwanja vya Chinangali, inahusisha uboreshaji wa Soko Kuu la Majengo, Kituo cha Daladala Mshikamano, Stendi ya mabasi madogo eneo la Kizota, ujenzi wa stendi ya mabasi madogo eneo la Nzuguni, pamoja na ujenzi wa vivuko katika maeneo ya Chadulu, Mailimbili, na Ntyuka.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mohamed Mchengerwa (Mb), aliwaomba watanzania kuitunza miradi hiyo inayotekelezwa kwenye majiji na miji zaidi ya 45 kwasababu ina thamani kubwa zaidi ya Trilioni 1.1.

Alisema kuwa mkataba huo wa bilioni 14.2 wa kuboresha na kujenga miradi ni matarajio ya kila mwanadodoma kuwa utaleta mapinduzi makubwa kiuchumi kwa watanzania na kuitunza miundombinu. “Ninawaomba watanzania simamieni miradi hii, ilikusudi iweze kuwasaidia watanzania wa karne hii na karne zinazokuja. Mnapoona wakandarasi wanalegalega tupeni taarifa, tuchukue hatua kwasababu miradi hii, Dkt. Samia Suluhu Hassan amewakusudia watanzania, sasa haiwezekani fedha hizi zote zitolewe na miradi itekelezwe kwa kiwango cha chini. Tumeshuhudia tukio la utiajia saini wa sehemu ya pili ya utekelezaji wa miradi, matarajio yetu usimamizi uwe wa kina” alisema Mchengerwa.

 


Aidha, Mchengerwa aliwaelekeza watendaji wa serikali chini ya TAMISEMI wasimamie miradi hiyo, wakipita sehemu wakakuta kuna changamoto ambazo watendaji hao walikuwa na uwezo wa kuzitatua watachukua hatua kwasababu jukumu kubwa ni kuitunza miundombinu inayojengwa.

 

Kwa upande wake, mfanyabiashara na  mkazi wa Nzuguni, Kuruthum Musse, alieleza furaha yake kubwa baada ya serikali kuwapelekea mradi wa ujenzi wa kituo cha daladala katika eneo lao kwa kuwa ujenzi huo ni hatua muhimu katika kuboresha huduma za usafiri na kupunguza changamoto kwa wananchi, kushushwa sehemu ambayo mazingira siyo rafiki. “Miundombinu tunayoenda kutengenezewa tunatakiwa tuitunze, tuiangalie, pia tuilinde hata ukiona mtu anataka kufanya chochote kwenye huo mradi lazima ukemee na unajua serikali ni mimi na wewe. Kituo hiki kitawasaidia abiria kupata usafiri kwa urahisi na kwa wakati. Naona matumaini makubwa kuwa mradi huu utaleta mabadiliko chanya katika maisha ya watu.” alisema Musse.

 

Nae, Mwanafunzi anayesoma stashahada ya Utendaji katika Chuo cha Serikali za Mitaa Dodoma, Kampasi ya Dodoma Mjini, Jafar Jamal, aliipongeza serikali kwa hatua waliyoichukua ya kusaini mkataba kwa sababu wananchi watanufaika na miradi hiyo itaondoa changamoto nyingi za usafiri kwenye maeneo yenye wingi wa abiria. “Binafsi kama mwananchi nitajitahidi kulinda miundombinu inayotekelezwa na serikali ili ilete manufaa kwetu. Lakini pia hii ni hatua muhimu kwa sisi wakazi wa Dodoma kwasababu tunahitaji miundombinu bora ili kuboresha maisha. Kwangu mimi natarajia kuona mabadiliko makubwa kwenye huduma za usafiri” alisema Jamal.

 


Mradi wa TACTIC ni mojawapo ya miradi inayofadhiliwa na serikali kuu kupitia mkopo wa Benki ya Dunia wenye thamani ya Dola za Kimarekani Milioni 410 (Bila VAT). Malengo ya mradi huu ni kuboresha miundombinu ya Tanzania Pamoja na kuzijengea uwezo taasisi (Halmashauri) ili ziweze kujiimarisha katika usimamizi wa uendeshaji miji pamoja na ukusanyaji wa mapato.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma