Wakandarasi Wasiomaliza Miradi Mashakani

Na. Faraja Mbise, DODOMA

TARURA imeagizwa kuwasimamisha wakandarasi wasiokamilisha miradi kwa wakati na wasipewe tena miradi hiyo kwasababu wanakwamisha juhudi za Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati na ya kimaendeleo nchini.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mohamed Mchengerwa (Mb)


Hayo yalisemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mohamed Mchengerwa (Mb) alipokuwa akizungumza na wataalam kutoka taasisi mbalimbali za kiserikali pamoja na wananchi wa Jiji la Dodoma katika Hafla ya utiaji saini mkataba wa uboreshaji Soko Kuu la Majengo pamoja na ujenzi wa Kituo cha Daladala eneo la Mshikamano, Kizota na Nzuguni, uliofanyika tarehe 06 Februari, 2025 katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.

“Maelekezo yangu kwa TARURA, mkandarasi huyu asiruhusiwe kufanya kazi yoyote chini ya TARURA kuanzia sasa mpaka akamilishe mradi huu tunaoukusudia. Nendeni makafanye tathmini, mniletee taarifa maramoja” alielekeza Mchengerwa.

Kauli hiyo, ilifuatiwa mara baada ya Waziri wa Madini, Anthony Mavunde (Mb) kutoa lalamiko la kutokukamilika kwa mradi uliokabidhiwa tarehe 23 Septemba, 2023, Mkandarasi huyo alipatiwa kiasi cha fedha Milioni 24 kwa awamu ya kwanza na kutakiwa kukamilisha mradi huo kwa wakati.

Sambamba na hilo alitoa agizo kwa wakandarasi wote nchini, ambao hawakamilishi miradi yao kwa wakati uliowekwa katika mikataba wasiruhusiwe kupewa kazi yoyote. “Mkandarasi huyu na wengine ambao hawajakamilisha miradi hii ambayo ilipaswa ikamilike mwezi Februari wasiruhusiwe kupewa kazi yoyote hata ya shilingi 500. Hatuwezi kuwa na watu ambao hawawezi kuona fikra za Rais wetu anatafuta fedha, analeta fedha, na bado wanakuwa goigoi hatuwezi kukubali hata kidogo. Maelekezo yangu kwa Mkandarasi huyu na wengine wa aina hii wasiruhusuiwe kufanya a kazi kokote ndani ya TARURA” aliagiza Mchengerwa.

Aidha, alitoa maelekezo mahususi kwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kuweka utaratibu mzuri wa watu wa kuingia na kutoka katika Stesheni ya reli ya mwendokasi (SGR), Samia Suluhu Hassan, Dodoma,  kwa sababu Jiji la Dodoma ndio makao makuu ya nchi.

“Ninawataka wakurugenzi wote wa majiji lakini hasa Jiji la Dodoma ambalo ndio makao makuu ya nchi, Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa wilaya nendeni mkajipange hasa pale eneo la Stesheni ya reli, utaratibu wa watu kuingia na kutoka haujakaa vizuri, makakae pamoja na TRC muweke utaratibu mzuri. Haieleweki na Rais wetu hawezi kutuelewa, yeye ameleta fedha, ninyi wajibu wenu ni kuwasaidia watanzania ili waweze kupata njia nzuri ya kuingia kwenye Stesheni ya reli. Sasa ninawataka ninyi na TARURA mkajipange vizuri, mkazungumzeni na wizara ya uchukuzi ili kuweka utaratibu watanzania wanaokwenda na kurudi kutoka Dodoma waweze kuingia na kupita vizuri eneo lile” alisema Mchengerwa.

Kwa upande wake Diwani wa Kata Ya Makole, Omar Omar, alimshukuru Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mkioa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa mikakati mizuri ya kuboresha miundombinu ya Jiji la Dodoma na kukemea wakandarasi wote ambao hawatekelezi miradi yao kwa wakati. Aidha, alitoa wito kwa wakandarasi kusimamia na kutekeleza miradi kwa wakati.

“Tumeona namna alivyokuwa anazungumza, kuonesha ukali namna ambavyo atataka kustawisha makao makuu ya nchi Dodoma, hususani katika suala la maendeleo  na upangiliaji wa mji wa Dodoma nampongeza pia kwakuwa amekuwa mkali kwa wakandarasi wavivu ambao wanapewa kazi na kutoweza kutekeleza kwa wakati. Rai yangu ninawasisitiza wakandarasi wote ambao wamepewa agizo hili waweze kufanya kazi zao kwa wakati na miradi kutekelezeka kwa wakati” alitoa rai Omar.

Nae mfanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo, Samiri Majid , aliunga mkono agizo la waziri Mchengerwa la kuwasimamisha wakandarasi wasiotekeleza miradi yao kwa wakati na akatoa rai yake kwa wakandarasi wote na kusisitiza watangulize uzalendo mbele badala ya maslahi yao binafsi.

“kwa upande wangu nianaona jambo hilo ni jema kwasababu wakandarasi wa namna hiyo wanachelewesha sana maendeleo ya taifa letu. Rai yangu kwa wakandarasi ni kwamba wakati wakikabidhiwa ‘share’ ya mradi wajitahidi kufanya kazi hiyo kama walivyokuwa wanahitaji kupewa kufanya hiyo kazi, kwasababu mkandarasi atakapokuwa anahitaji kupata ‘share’ atatumia mbinu yoyote ile kuhakikisha anapata. Hivyo niwaombe watangulize uzalendo mbele, maslahi ya nchi mbele na wasitangulize maslahi yao binafsi ili taifa letu lizidi kukua na kuwa taifa linalojengeka kadri siku zinavyokwenda” alisema Majid.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma