Sekta binafsi kugharamia miradi Jiji la Dodoma Bajeti ya 2025/2026

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Sekta binafsi itashiriki kugharamia miradi ya maendeleo kwa njia ya ubia katika utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Halmashauri kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 kutokana na umuhimu wa sekta hiyo kwa maendeleo ya Jiji la Dodoma.


Katibu wa Baraza la Madiwani, Dkt. Frederick Sagamiko


Mapendekezo ya Rasimu ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, imeshirikisha sekta binafsi kutokana na matamanio na mahitaji kuwa makubwa kuliko makusanyo ya mapato.

Hayo yalisemwa na Katibu wa Baraza la Madiwani ambaye ni Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko, alipokuwa anatolea ufafanuzi katika baadhi ya masuala yaliyowasilishwa katika Mkutano wa Baraza la Madiwani maalum kwa ajili ya kupokea na kupitia mapendekezo ya rasimu ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2025/26 katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma tarehe 30 Januari, 2025.

Dkt. Sagamiko alisema “matamanio yetu na mahitaji yetu ni makubwa kuliko makusanyo yetu ndio maana kwenye bajeti hii kipekee kabisa tunaweza kushirikisha sekta binafsi katika ugharamiaji wa Mpango na Bajeti kwa mwaka wa Fedha 2025/2026 ile tuliyoiita ubia ‘PPP”.

Akizungumzia kuhusu utekelezaji wa Mpango na Bajeti hiyo, alisema kuwa, kuna miradi mingi ya kuvutia ambayo itashawishi wawekezaji kushirikiana nao katika utekelezaji. “Ipo miradi mingi ambayo ni ya kuvutia sana ambayo tunaamini kabisa itaongeza ‘appetite’ kwa wawekezaji kuja kushirikiana nasi katika utekelezaji wa Mpango na Bajeti hii kama miradi ilivyoainishwa pale” alisema Dkt. Sagamiko.

Kuhusu ukamilishaji wa miradi viporo, alisema kuwa, dhamira ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kupitia bajeti hiyo itaenda kukamilisha miradi yote viporo. “Dhamira yetu ni kwamba, bajeti ya Mwaka wa Fedha 2025/2026 inaenda kukamilisha miradi yote viporo, haijalishi mradi huo ulipelekewa fedha za Serikali Kuu lakini haikutosha au ulianzishwa kwa nguvu za wananchi, tunahakikisha miradi yote inaenda kuisha. Ile milioni 150 tunayoiongelea haiendi kugusa miradi viporo, miradi viporo imetengewa shilingi bilioni 7.1” alisema Dkt. Sagamiko.

Sambamba na hilo alisema kuwa wamelenga katika kusogeza huduma karibu na wananchi ikiwemo za ardhi, vibali vya ujenzi, na huduma zote zinazopatikana ofisi kuu ili wananchi wasiweze kufuata huduma hizo umbali mrefu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe, alisema kuwa Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2025/2026 ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma inalenga kukamilisha miradi viporo katika jumla ya kata 41 za halmashauri hiyo.




Kwa mwaka huu, Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma ambayo inafikia takribani shilingi Bilioni 147 inalenga kwenda kukamilisha miradi viporo katika kata zetu 41. Viporo ni miradi ambayo haikuisha kwa wakati kutokana na namna ya kuibuliwa na sisi wenyewe na serikali kwa ujumla na viporo vingine kuibuliwa na wananchi wenyewe. Kwahiyo tumetenga kiasi cha Bilioni 7.1 ili iweze kwenda kukamilisha hivyo viporo” alisema Prof. Mwamfupe.

Nae, Diwani wa Viti Maalum Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Wendo Kutusha alipongeza wasilisho la bajeti lililotolewa kwa kutenga fedha kwa ajili ya umaliziaji wa miradi viporo kwa Kata zote za Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Tumeona kwamba bajeti hii imetenga kiasi cha shilingi Bilioni saba kwa ajili ya kumalizia miradi yote viporo. Katika kata zetu kuna miradi ambayo ni ya serikali na iliyoibuliwa na wananchi, miradi hiyo imekuwa ikitesa sana huko kwa pesa kidogo, inaenda kwa ‘speed’ ndogo lakini bajeti yetu inaenda kujibu na kumaliza matatizo yote” alipongeza Kutusha.

Vilevile, Diwani wa Kata ya Mkonze, David Bochela, aliondoa dhana iliyokuwepo kwa muda mrefu ya Jiji la Dodoma kutegemea mapato ya ardhi na alisema kupitia miradi iliyowasilishwa, Jiji la Dodoma litaenda kukusanya mapato kwa wingi. “Ilidhaniwa wakati fulani kwamba Jiji la Dodoma linategemea mapato ya ardhi lakini tunakwenda kutoka huko kwenye picha ya viwanja, kupitia miradi mikubwa ya utekelezaji jiji letu litakusanya mapato mengi na kwa maana hiyo tutakuwa na mapato mengi” alisema Bochela.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma