Jiji la Dodoma linafursa lukuki uwekezaji

 Na. Faraja Mbise, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma inazo fursa lukuli kwa ajili ya wawekezaji na wafanyabiashara katika maeneo ya kilimo, viwanda, biashara, michezo na maeneo mengine yanayoweza kusisimua ukuaji wa uchumi.


Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma, Abdul Chacha alipokuwa akizungumza na wajumbe wa Mkutano wa Baraza la Biashara Wilaya ya Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma uliopo Mji wa Serikali Mtumba. “Halmashauri ya Jiji la Dodoma ina fursa nyingi sana, una fursa ya kuwekeza katika maeneo ya michezo kwa ujumla, kwasababu saizi tunaangalia AFCON inakuja. Kwahiyo, watu wengi watahitaji sehemu ambazo zimeandaliwa kwa ajili ya michezo. Vilevile, nyumba za kupanga na kuuza (apartment). Kipindi hiki wageni wanaingia wengi sana hivyo, wanahitaji sehemu za kufikia kwa maana ya malazi, hizo ni fursa zinazopatina. Lakini biashara mbalimbali za chakula kama kuku, nyama, mbogamboga na matunda ni mahitaji katika soko la Jiji la Dodoma. Sasa hivi, mtaona magari mengi ambayo yalikuwa yanatoka mikoani yanaenda Dar-es-Salaam yanashusha bidhaa zao hapa Dodoma. Kwahiyo, hata mzunguko wa pesa umeongezeka mara dufu tofauti na ilivyokuwa zamani” alisema Chacha.

Akiongelea utatuzi wa changamoto, alisema kuwa baraza hilo limekuwa msaada mkubwa. “Changamoto nyingi tumeweza kuzitatua. Mfano, wafanyabiashara wanalalamika kuhusu ushuru au kodi zilizowekwa ambazo hawazifahamu, lakini baada ya kukutana nao katika vikao vyetu, tunawafahamisha zile kodi zimewekwa kwa utaratibu gani, malengo yake ni yapi. Wafanyabiashara wamekuwa wakielewa na utaratibu unaendelea. Pia changamoto nyingine tuna wafanyabiashara wadogo na wa kati, wafanyabiashara wadogo mfano machinga wanachangamoto ya maeneo ya kufanyia biashara. Hivyo, tunakaa nao na kuongea na kukubaliana mambo ya msingi. Baraza hili kupitia halmashauri wataandaliwa maeneo maalumu ambayo utaona wanapewa yakiwa na huduma zote za msingi ili waweze kutoa huduma zao” aliongeza Chacha.

Akiongelea ujio wa reli ya kisasa (SGR) alisema kuwa imesaidia kukuza biashara katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Kitakwimu bado tunaendelea kufanya tafiti zetu, lakini kiwango kikubwa sana mtaona ‘movement’ ya watu kwenda Dar-es-Salaam na kurudi ni kubwa zaidi. Hii imefanya biashara katika Jiji la Dodoma isiwe na tofauti kubwa na ile iliyopo katika Jiji la Dar-es-Salaam kwasababu zinapatikana kwa wepesi na gharama nafuu kwasababu wafanyabiashara hawatumii muda mrefu sana kufuata bidhaa zao” alisisitiza Chacha.

Mkuu huyo wa Divisheni ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara aliwataka wafanyabiashara na watanzania kwa ujumla kulipa kodi kwa uaminifu ili kuleta maendeleo katika nchi. “Tumeendelea kuwaelimisha na kuwahamasisha watanzania kwa ujumla kwamba kodi zao ndio zinazojenga nchi, upatikanaji wa kodi zao ndio unaofanya maendeleo yote yanayoonekana sasahivi yanatokana na kodi zao. SGR ni kodi zao, miundombinu, barabara, huduma za kijamii, huduma za afya zote zinaweza kufanyika kwasababu ya kodi zao. Kwahiyo, mchango wa kodi ya wananchi ni muhimu sana kwa maendeleo” alisisitiza Chacha.

Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma linahusisha wafanyabiashara kutoka sekta ya umma na sekta binafsi kwa lengo la kujadili masuala ya biashara na uwekezaji kwa mapana, changamoto na utatuzi wake, muelekeo na namna ya kufikia maelengo ya halmashauri, wilaya, mkoa na taifa kwa ujumla.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma