Ukarabati Shule ya Msingi Iyumbu kupunguza msongamano darasani

Na. Dennis Gondwe, IYUMBU

MRADI wa ukarabati wa vyumba 10 vya madarasa katika Shule ya Msingi Iyumbu umesaidia kupunguza msongamano wa wanafunzi darasani na kuwaboreshea wanafunzi mazingira bora ya kujifunzia.


Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Iyumbu, Mwl. Monica Nshimba


Kauli hiyo ilitolewa na Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Iyumbu, Mwl. Monica Nshimba alipokuwa akisoma taarifa ya mradi wa ukarabati wa vyumba 10 vya madarasa katika Shule ya Msingi Iyumbu kwa Kamati ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dodoma ilipotembelea shule hiyo iliyopo Kata ya Iyumbu jijini Dodoma.


Mwl. Nshimba alisema “ukarabati wa mradi umepunguza kwa kiasi kikubwa msongamano wa wanafunzi darasani kwasababu kabla ya ukarabati, kulikuwa na vyumba vinne ambavyo vilikuwa havitumiki kabisa na hata vile vilivyokuwa vinatumika vilikuwa katika hali mbaya sana. Hivyo, kwa sasa vyumba vyote vinatumika. Pia mazingira ya kujifunzia na kufundishia yamekuwa mazuri na rafiki kiasi kwamba wanafunzi na walimu wote tunayafurahia. Hivyo, kuongeza ari ya kufanya kazi na kujifunza”.


Akiongelea mapokezi ya fedha, alisema kuwa shule yake ilipokea fedha kiasi cha shilingi 90,000,000.00 kutoka Serikali Kuu tarehe 05 Januari, 2024 kwa ajili ya ukarabati wa vyumba 10 vya madarasa. “Mradi huu ulianza kutekelezwa tarehe 15 Januari, 2024 na umetekelezwa kwa kutumia ‘Force Account’ ambapo kulikuwa na kamati tatu za Ujenzi, Manunuzi na Kamati ya Mapokezi na Ukaguzi. Kamati hizi zilikuwa na uwakilishi wa wananchi wa Kata ya Iyumbu ambao wameshiriki katika usimamizi wa mradi hadi kukamilika. Mradi umetumia jumla ya shilingi 90,000,000.00 ambapo imejumuisha malipo ya wazabuni, fundi na kodi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Mradi umekamilika kwa asilimia 100 uliohusisha ukarabati wa vyumba 10 vya madarasa na ofisi mbili umekamilika tarehe 30 Aprili, 2024 na mradi unatumika” alisema Mwl. Nshimba.

 


Ikumbukwe kuwa Shule ya Msingi Iyumbu ilianzishwa mwaka 1980 sasa ina wanafunzi 1,219 kati yao wavulana ni 561 na wasichana ni 658 ikijivunia kufanya vizuri kitaaluma kwa kuongeza ufaulu kwa darasa la Saba kwa miaka mitatu mfululizo.

MWISHO  

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma