Kituo cha Afya Ilazo kuboresha huduma ya mama na mtoto

Na. Dennis Gondwe, NZUGUNI

MRADI wa ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo utawezesha kutoa huduma za upasuaji, kliniki ya mama na mtoto na huduma za kujifungua zikiwa zimeunganishwa na mfumo wa hewa ya Oksijeni.



Kauli hiyo ilitolewa na Kaimu Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma, Dkt. Revocatus Baltazary alipokuwa akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo kwa Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Dodoma ilipotembelea na kukagua miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.


Dkt. Baltazary alisema “mradi huu utawezesha kutoa huduma za upasuaji, kliniki ya mama na mtoto, huduma za kujifungua, wodi ya watoto wachanga, huduma za kuhifadhi miili. Wodi hizi pia zimeunganishwa na mifumo ya hewa ya Oksijeni ambayo ipo katika wodi ya wazazi, watoto na jengo la upasuaji. Mifumo hii itasaidia wagonjwa wote wenye changamoto ya upumuaji kupata huduma hapa kituoni.  Aidha, huduma za lishe zitatolewa ikiwemo elimu juu ya masuala ya lishe, upimaji wa hali za lishe na ushauri”.


Akiongelea lengo na gharama za mradi huo alisema ni kuboresha huduma za mama na mtoto na huduma za upasuaji. “Gharama ya mradi huu hadi utakapokamilika ni shilingi 3,094,983,663.32 kati ya fedha hizo shilingi 2,870,483,663.32 ni gharama za ujenzi na shilingi 224,500,000.00 ni kwa ajili ya mshauri mwelekezi na hadi hatua hii iliyofikia kiasi cha shilingi 2,583,435,296.98 kimetumika. Kwa sasa Jiji la Dodoma limepokea baadhi ya vifaa tiba vitakavyotumika katika mradi huu kutoka Shirika la kimataifa la kuhudumia watoto (UNICEF). Pia watumishi 17 watakaotoa huduma katika kituo hiki wameshajengewa uwezo na kwa hivi sasa wako katika vituo mbalimbali wakiendelea kuongeza uzoefu” alisema Dkt. Baltazary.





Mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo unajengwa chini ya ufadhili wa KOICA kupitia Shirika la kimataifa la kuhudumia watoto UNICEF, ukiwa unatekelezwa katika Kata ya Nzunguni, Mtaa wa Ilazo ukitarajiwa kuhudumia wananchi zaidi ya 99,743.

 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma