Shule ya kwanza ya Sekondari yajengwa Matumbulu tangu Uhuru

Na. Nancy Kivuyo, MATUMBULU

Diwani wa Kata ya Matumbulu, Emmanuel Chibago aishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha miundombinu katika sekta ya elimu katani hapo.


Diwani wa Kata ya Matumbulu, Emmanuel Chibago, akitoa shukrani kwa rais

Alitoa shukrani hizo wakati alipokuwa mwenyeji wa waandishi wa habari waliotembelea miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na serikali kuanzia mwaka 2020 hadi 2025 katika Kata ya Matumbulu.

 

Chibago alisema kuwa ni historia kwa Kata ya Matumbulu kuwa na shule ya sekondari na kusema kuwa haijawahi kutokea tangu kupatikana kwa uhuru. “Kiukweli, nampongeza sana Rais wetu pamoja na Mbunge Mavunde, wamehakikisha wananchi tunaoishi hadi pembezoni mwa mji tunapata shule ili watoto wetu wapate elimu nzuri. Ukitazama ndugu mwandishi, haya majengo ni ya kisasa kabisa, wanafunzi watasoma katika mazingira mazuri na italeta chachu ya ufaulu kwasababu kule msingi walipo sasa hivi watasoma kwa bidii ili wafaulu waje sekondari” alisema Chibago.

“Serikali yetu ni sikivu, tuliomba tujengewe shule hapa na tumeletewa kiasi cha shilingi 544,000,000 kupitia mradi wa SEQUIP, ndio matunda yake haya tunaiona shule ipo mbioni kukamilika. Tuna kila sababu ya kujivunia sekondari hii na tutaitunza kwa namna ya kipekee kuhakikisha kwamba inafaa kwa vizazi vyetu na hata vya baadae” alisisitiza Chibago.




Nae Afisa Elimu Kata ya Matumbulu, Ally Mgoo aliishukuru serikali kwa kujenga shule katani hapo kwasababu itasaidia wanafunzi waliokua wanaenda kata jirani kusoma kubaki hapo na kupata elimu. “Serikali yetu kupitia rais, mbunge na diwani wamefanya jambo la msingi kuipa kipaumbele sekta ya elimu katika kata yetu. Watoto walikua wanatembea mbali kwenda kusoma, kuna ambao walikatiza masomo sababu ya umbali, wapo waliokumbana na vishawishi wakapata mimba na kuacha masomo. Hivyo, ujio wa shule hii utaboresha elimu katika eneo hili na tunategemea kupata wasomi wengi” alishukuru Mgoo.

 

Katika hatua nyingine Vicent Yohana aliipongeza serikali kwa kufanya maboresho katika sekta ya elimu na kuiwezesha kata kupata shule ya sekondari. “kwakweli, tunaipongeza serikali kwa kutuletea maendeleo katika elimu, watoto wetu sasa watasoma katika mazingira mazuri na ninaamini watafaulu. Hii shule ni mfano mzuri wa maendeleo mengine katika kata yetu. Tunashukuru sana kwa hili” alishukuru Yohana.




MWISHO

 

 

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

RC Senyamule azipongeza Club za Jogging Dodoma

Usafi wa Mazingira Kipaumbele Kata ya Chamwino