Kongamano kuhamasisha wanawake kugombea nafasi za uongozi lafanyika Dodoma

Na. Nancy Kivuyo, DODOMA

Kongamano la kanda ya kati likihusisha mikoa ya Dodoma, Singida na Iringa lilifanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete huku kaulimbiu ikiwa ‘Wanawake na Wasichana 2025: Tuimarishe Haki, Usawa na Uwezeshaji’.



Katika kongamano hilo, mada chokozi inayosema “Wanawake na Uongozi katika miaka 30 ya Beijing” iliandaliwa ambapo wanawake mashuhuri walialikwa kujadili mada na kutoa shuhuda mbalimbali za namna walivyoweza kufaulu katika harakati za kuwa viongozi na kushika nyadhifa mbambali nchini.

Akizungumza na maelfu ya wanawake waliohudhuria katika kongamano hilo mgeni rasmi Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anna Makinda alisema “wanawake changamkieni fursa za uongozi kwasababu hata sisi tumekua mfano kwenu, angalieni mheshimiwa rais wetu ni mwanamke anaiongoza nchi hii bila hofu, nyie mnashindwa hata kugombea udiwani?. Akina mama amkeni, awamu hii tunaelekea kwenye uchaguzi hivyo tunawategemea uwakilishi kwenye ubunge, udiwani na nafasi zingine”.  

Nae Rhobi Maro aliyehudhuria kongamano hilo alisema alifurahi kuhudhuria na kwamba alipata maarifa mengi na uthubutu wa kufanya maamuzi. Aliongeza kuwa “naamini wanawake wengi watajitokeza kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi ujao sababu uwezo huo wanao na natumai itakua hivyo”.



Kwa upande mwingine, Evelyn Alphonce alizungumza kuwa “siku ya leo imekua siku muhimu sana kuelekea kilele cha Siku ya Wanawake Duniani, nimefurahi kukutana na watu tofauti tofauti na kubadilishana nao mawazo, niseme tu nimehamasika”.

Kongamano hilo lilihudhuriwa na wanawake wengi kutoka taasisi mbalimbali ikiwa ni shamrashamra za kujiandaa kuelekea kilele cha madhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kinachotarajiwa kufanyika kitaifa Machi 8 mkoani Arusha ambapo mgeni rasmi atakua Rais wa Jamhuri ya Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Bilioni 9.1 yanufaisha vikundi kwa Mwaka 2020-2023

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma