Jiji la Dodoma latoa elimu dhidi ya ukatili wa kijinsia kwa wanafunzi wa kike

Na. Nancy Kivuyo, DODOMA

Ofisi ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kupitia Divisheni ya Maendeleo ya Jamii, walitoa mafunzo kwa wanafunzi wa Shule za Sekondari Viwandani na Kikuyu ikiwa ni shamrashamra za kueleka kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani itakayofanyika kitaifa mkoani Arusha tarehe 08 Machi, 2025.




Akizungumza na wanafunzi wasichana kwenye shule hizo, Afisa Maendeleo ya Jamii, Dawati la Msaada wa Kisheria, Elizabeth Godwin alisema “tupo katika kuhakikisha binti anapata elimu kuhusiana na masuala ya ukatili wa kijinsia kwasababu tunaamini ya kwamba, binti anapofanyiwa ukatili wa kijinsia ndio tunapoteza ule uhalisia wa mwanamke ambae baadae ndio angekuja kuwa nguzo muhimu ya familia kama mlezi au mzazi mzuri. Tushukuru Mungu wanafunzi wameitikia wito wa elimu hii nzuri, wameonesha kuelewa juu ya elimu ya ukatili na mahali gani pa kuripoti”.

Nae Mratibu wa Elimu Kata ya Viwandani, Zaituni Mkoyi aliwaasa wasichana wanafunzi kuzingatia masomo ili waje kuwa mfano mzuri katika maisha yao ya sasa na ya baadae. “Hata sisi tulikua watoto kama ninyi, lakini tulisoma kwa bidii na kuchangamkia fursa mbalimbali ndio maana mnatuona leo hapa. Hata nyie mnaweza, msome kwa bidii, muwe watoto wasikivu, muwe na heshima kwa wazazi na wakubwa zenu na hakika mtafanikiwa” alisema Mkoyi.

Kwa upande mwingine, Mwanafunzi Conjesta Mwanika alisema kuwa amejifunza vitu vingi katika mafunzo hayo na anaamini atasoma kwa bidii na kufuata ushauri makini uliotolewa. “Nimejifunza vitu vingi sana leo, la kwanza tuzingatie masomo, tuwe na nidhamu, tuchangamkie fursa za kujishughulisha na kilimo cha vitalu, kufanya biashara ndogo ndogo ili kujikimu na kukwepa tamaa” alisema Mwanika.

Nae Mwanafunzi, Jenipha Mandela alishukuru kwa mafunzo hayo na kuahidi kusoma kwa bidii ili kuweza kufikia ndoto zake. Aliongeza kuwa amepata elimu kubwa juu ya masuala ya ukatili wa kijinsia na kusema “ukatili wa kijinsia unaweza kutuathiri kisaikolojia, hivyo tunapaswa kuripoti matendo mabaya kwa mwalimu wa Malezi au jirani ambae ni mshauri mzuri ili aweze kutusaidia katika kutatua tatizo hilo” alisema Mandela.






MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Bilioni 9.1 yanufaisha vikundi kwa Mwaka 2020-2023

Halmashauri ya Jiji la Dodoma yatoa Kongole kwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan