Wananchi Dodoma watakiwa kuzingatia vibali vya ujenzi

Na. Halima Majidi, VIWANDANI


Wananchi jijini Dodoma wametakiwa kuacha tabia ya ujenzi wa aina yoyote bila ya kufuatilia vibali kwa sababu ni kosa la kisheria na linaweza kusababisha ujenzi holela na migogoro ya Ardhi isiyo ya lazima.



Hayo yalisemwa na Msanifu Majengo wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Paschal Mathew wakati akitoa elimu juu ya umuhimu wa vibali vya ujenzi kwa wananchi wanaotaka kujenga ikiwa ni muendelezo wa Kliniki ya Ardhi inayofanyika jijini hapo katika viwanja vya iliyokuwa Manispaa ya zamani.

Alisema kuwa vibali vya ujenzi wanatoa kwa mujibu wa sheria, na kwa viwanja vyote ambavyo vimeshafanyiwa vipimo na kumilikishwa ili mwananchi apewe huduma, lazima awe na nyaraka za umiliki pamoja na michoro ya majengo anayotaka kuendeleza yakizingatia matumizi na sheria ndogo za Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Tunakagua michoro kuangalia kama imekamilika na imekidhi vigezo vya kihandisi na kisanifu na kuwaandikia “invoice” kwaajili ya kufanya malipo ya kibali cha ujenzi. Baada ya kulipia wataalamu watapitia michoro na kibali chake kwa lengo la kujiridhisha” alisema Mathew.

Aidha, alifafanua kuwa muamko wa wananchi ni mkubwa ila kuna changamoto ya uelewa, kuna mwingine anakuja kuomba kibali akiwa na nyaraka ila hana michoro ya ujenzi. “Tunampa elimu kwanza ya namna gani afanye, awasiliane na wataalamu wa aina gani ili aweze kuandaliwa michoro yake kisha aje na michoro hiyo ili tuweze kumpa kibali. Mpaka leo tarehe 26 Februari tumepokea zaidi  ya maombi ya vibali vya uendelezaji ujenzi 20, ambapo bado tunaendelea na huduma hiyo” alifafanua Mathew.

Nae, Epimark Madole ambae ni mkazi wa eneo la Mipango alipongeza huduma za utoaji wa vibali, kwa sababu inasaidia kujenga katika sehemu husika na kuepusha migogoro na Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Tunapaswa kuzingatia taratibu zote za jiji kuhusiana na vibali vya ujenzi, usijenge kabla ya kuomba kibali cha ujenzi, unatakiwa ufuate taratibu ikiwemo kuwa na michoro iliyokaguliwa na kulipia ili kuepuka malumbano na Jiji la Dodoma” alisema Madole.  

Sanjari na hayo alisema kuwa mtu akijenga bila kupata kibali anaweza kujenga sehemu ambayo sio rasmi ikiwemo barabarani kwa sababu anakuwa hajazingatia mipaka. “Unaweza ukajenga eneo ambalo lilitakiwa kujengwa makazi wewe ukajenga ‘commercial’ au maduka. Kwa hiyo, lazima kuzingatia kwa kufuata sheria ili kuepusha usumbufu wa kubomolewa majengo yetu” alisema Madole.

Kwa upande wake Fausta Kusakala alisema kuwa changamoto yake ni kiwanja chake kilichopo Chinangali West ambapo kila akiingia kwenye mtandao anaambiwa kiwanja kimefutwa. “Kwa ujumla huduma ni nzuri, nimeambiwa niende kwa Kamishna kwaajili ya hitimisho” alisema Kusakala.

MWISHO

 

 

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma