Prof. Mwamfupe; Taka ni fursa ya kutengenezea mbolea

 Na. Aisha Haji, DODOMA

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe, amewataka wananchi kuendelea kutunza mazingira na kutumia takataka zinazotokana na mazao kama fursa ya kutengeneza mbolea ili kuweza kuinua sekta ya kilimo na uchumi wa halmashauri kiujumla.




Aliyasema hayo katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wakati wa majadiliano na Kamati ya Ushauri ya Wilaya iliyokutana kupitia mapendekezo ya Mpango na Bajeti ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Akizungumza kuhusu umuhimu wa mbolea zitokanazo na takataka za mazao, alisema kuwa taka za mazao ambazo zinaoza kwa urahisi ni fursa nzuri sana ya kiuchumi kuweza kutengeneza mbolea. Pia alidokeza kuwa halmashauri imejipanga katika suala la kutoa mikopo, mafunzo na ushauri wa kitaalamu kwa wananchi kuhusu namna ya kutumia taka zitokanazo na mazao kwa ajili ya kutengeneza chakula cha kuku kwa kufuata utaratibu maalumu.

Prof. Mwamfupe alisema “halmashauri itakuwa tayari kupitia taratibu zake za kutoa mikopo lakini vilevile, kutoa ushauri wa kitaalamu wa namna ya kutumia taka zinazotoka kwenye masoko yetu kwa ajili ya kutengeneza chakula cha kuku”.

Aidha, aliongeza kuwa wajumbe wajitokeze katika kuchangia  maoni na ushauri katika kikao cha kamati ya ushauri ya wilaya ili kutambua mambo mbalimbali yanayowakumba wananchi na kupendekeza masuluhisho. “Ningetamani sana michango ya watu kama hivi iweze kujitokeza mara kwa mara. Michango hii tunayoipata hapa tunafurahi kwamba tungekuwa tumepata hata kabla ya wakati huu kwenye vikao vingine kwa ajili ya kuongelea maslahi ya wananchi” alisema Prof. Mwamfupe.

Sambamba na hayo alifafanua kuwa kuna umuhimu wa kuzingatia suala la kupanga bajeti katika mambo mbalimbali kwasababu bajeti yeyote inaundwa kwa kujumuisha mapato na matumizi. “.....bajeti inaundwa na hesabu ya makusanyo sawasawa na matumizi yaani kukiwa na senti moja, senti ishirini imezidi upande mmoja hiyo bajeti imeshindwa” alisema Prof. Mwamfupe.

Vilevile, alitoa rai kwa wajumbe na wananchi wote kwa ujumla kushirikiana na kuhamasishana katika suala la kulipa kodi, kukata leseni na kuchangia michango katika vyanzo mbalimbali vya mapato ili kukamilisha vizuri bajeti ya serikali.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma