Dodoma Jiji U-20 yakita Kambi Kileleni

Na. Mussa Richard, DODOMA

Klabu ya soka ya Dodoma Jiji chini ya umri wa miaka 20 (U-20) imeendeleza ubabe kwa wapinzani wake wanaoshiriki ligi ya vijana ya NBC chini ya umri wa miaka 20 Tanzania bara baada ya kuwashushia kichapo cha mabao 2-1 wanajeshi wa mpakani Mashujaa FC U-20, katika mchezo uliovulumishwa katika nyasi za dimba la Jamhuri Dodoma hapo jana.




Baada ya mchezo kutamatika kocha wa Dodoma Jiji U-20, Jeremiah Chido alisema “mchezo umemalizika salama na tumepata kitu ambacho tulikua tunakihitaji ambacho ni alama tatu muhimu. Alama ambazo zinatufanya tuendelee kuwa kileleni katika kundi letu na kutufanya tusicheze kwa presha michezo inayokuja mbele yetu, michezo ambayo tutakuwa ugenini”.

Katika hatua nyingine Chido akaweka wazi malengo yao kwenye msimu huu wa Ligi ya Vijana ya NBC Tanzania Bara. “Malengo yetu msimu huu ni kuchukua ubingwa kwasababu msimu uliopita tulifika fainali ila bahati haikuwa upande wetu. Kwahiyo, msimu huu tukishirikiana halmashauli, mashabikii, wachezaji na makocha mbalimbali hapa Dodoma nina uhakika tutachukua ubingwa wa Ligi hii ya vijana kwasababu rasilimali muhimu kwenye mpira ambayo ni wachezaji tunao na wanaonesha kila nia ya kuhitaji ubingwa” alisema Chido.

Kwa upande wake mchezaji wa Dodoma Jiji U-20, Christopher Shija ambaye ndiye kinara wa upachikaji mabao mpaka sasa katika ligi hiyo akiwa na mabao matano baada ya kumalizika kwa mchezo huo alisema malengo yake ni kuhakikisha anatwaa tuzo ya mfungaji bora wa ligi hiyo.

Namshukuru Mungu mpaka sasa naongoza katika orodha ya wafungaji na sijaridhika bado nitaendelea kutumia nafasi kila nikizipata ili niweze kuwa mfungaji bora. Lakini pia niwashukuru sana wachezaji wenzangu kwasababu bila wao kunitengenezea nafasi nisingekuwa nafunga. Kwahiyo, tukiendelea kuwa na ushirikiano ndani na nje ya uwanja tutafanikiwa katika malengo yetu kama timu na mchezaji mmoja mmoja” alisema Shija.




Baada ya ushindi huo Dodoma Jiji U-20 imefanikiwa kukusanya alama 22 kibindoni ikishuka dimbani katika michezo tisa ikibakisha michezo mitano kumaliza hatua ya makundi, huku ikiendelea kushika usukani katika kundi A. Katika michezo iliyosalia Dodoma Jiji U-20 inahitaji walau alama mbili ili kujihakikishia kufuzu hatua ya robo fainali ya ligi hiyo ambayo inachezwa katika mfumo wa makundi mawili ambapo nafasi ya kwanza hadi ya nne kwa kila kundi moja kwa moja zinatinga katika hatua ya robo fainali.




MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma