Twende Butiama wakabidhi Madawati 100 SM Dodoma Makulu

Na. Asteria Frank, DODOMA MAKULU

 

Watu wasiopungua 90 washiriki kwenye msafara wa Twende Butiama wakiendesha baiskeli kutoka Dar-es-Salaam na kwenda Butiama kwa lengo la kumuenzi Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Nyerere waliwasili jijini Dodoma katika Shule ya Msingi Dodoma Makulu na kugawa madawati 100 na kushiriki zoezi la kupanda miti.

 




Msafara huo ulianza safari tarehe 30 Septemba kutoka Dar-es-Salam na unatarajiwa kufika Butiama tarehe 13 Oktoba, 2024 ukidhaminiwa na Vodacom pamoja na Benki ya Stanbic walikabidhi madawati 100 na kupanda miti katika Shule ya Msingi Dodoma Makulu.

 

Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Kaspar Mmuya aliupokea msafara huo wa Twende Butiama na alisema kuwa, upandaji miti unaunga falsafa ya kutunza Mazingira. Alisema kuwa utoaji wa madawati shuleni unaugana na falsafa ya Mwl. Julius Nyerere ya kuangamiza maadui watatu wa maendeleo ikiwemo ujinga, umasikini na maradhi.

 

Alisema kuwa, kitendo wanachofanya ni kizuri kwa Tanzania cha kumuenzi Baba Taifa kwa kuendesha Baiskeli kutoka Dar-es-Salaam mpaka Butiama kinaonesha uzalendo. “Nimeambiwa safari hizi zimefanyika zaidi ya miaka sita huku mkisema tunamuenzi Baba wa Taifa kwa vitendo ni ukweli nimeona wakati ulivyokuwa unatambalisha hapa sio Tanzania tu ni zaidi ya Tanzania na hayo ndio maisha alikuwa akiishi Mwl. Julias Kambarage Nyerere hakuwa mbinafsi, alikuwa anapenda umoja” alisema Mmuya.

 

Aidha, Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhili Chibago alisema kuwa Jiji la Dodoma tumefarijika sana kwa kuwapokea Twende Butiama kwa baiskeli kwakuwa wamefanya kitu kizuri na kwa zoezi la kupanda miti kwa maana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluh Hassan na Makamu wa Rais watamani Dodoma iendelee kuwa kijani.

 

Alisema kuwa upandaji wa miti unaunganisha falsafa ya viongozi wa nchi. Kitendo cha kupeleka madawati kitawafanya watoto wanaposoma waelewe vizuri. “Tunawashukuru na tuwakaribishe sana Dodoma kwakuwa Dodoma ni fahari ya watanzania na ni mahali pa kuishi. Pia Zabibu nzuri inapatika huku karibuni sana” alisema Chibago.

 



Nae Mwenyekiti wa Msafara wa Twende Butiama, Gabriel Landa alisema kuwa wanatarajia kufika Butiama tarehe 13 Oktoba, 2024 kwa lengo la kumuenzi Hayati Baba wa Taifa kwa vitendo na kwaajili ya kuadhimisha miaka 25 ya kumbukizi ya kifo chake tarehe 14 Oktoba, 2024.

 

Alisema kuwa Msafara huo umezingatia jinsi zote mbili ya wanawake na wanaume bila kusahau watoto chini ya miaka 20. Pia umejumuisha waendesha baiskeli kati yao Tanzania Bara kutoka Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Tabora, Mbeya, Iringa, Geita, Mwanza, Katavi na Dodoma. Kwa upande wa Tanzania Visiwani ni Uguja na Pemba. Nchi jirani za Kenya, Burundi, Malawi na Congo zinashiriki, aliongeza.

 

“Kuna falsafa nyingi sana alituachia Baba wa Taifa na moja wapo ya kupambana na maadui watatu wa maendeleo ambao ni ujinga, umasikini na maradhi. Tumekuwa tukifanya  hayo kwa kipindi chote  tangia tumeanza mwaka 2019 na kupitia wadau mbalimbali tumeweza kukabidhi madawati zaidi ya 1,000 katika shule zaidi ya 13 hadi kufikia mwaka jana. Lakini pia tumeweza kupanda miti zaidi ya 50,000 na kuhamasisha watanzania kujali afya” alisema Landa.

 

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Dodoma Makulu, Mwl. Amon Sebyiga alisema kuwa anawashukuru Twende Butiama kwa kutukabidhi madawati 100 kati ya madawati 212 yaliyo kuwa pungufu katika shule yake.

 

Alisema kuwa madawati hayo yataenda kupunguza msongomano wa wanafunzi kukaa watano kwenye dawati moja. “Jamii ya Dodoma Makulu na watu wanaozunguka eneo hili nawatakia safari njema ndugu zetu wa Twende Butiama” alisema Mwl. Sebyiga. 

 

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma