Twende Butiama kupambana na ujinga, umasikini na maradhi Jiji la Dodoma

Na. Faraja Mbise, DODOMA MAKULU

Waendesha baiskeli wamuenzi Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Nyerere kwa lengo la kupambana na maadui watatu wa maendeleo ambao ni maradhi, umasikini na ujinga kwa kugawa madawati 100 katika Shule ya Msingi Dodoma Makulu iliyopo Halmashauri ya Jiji la Dodoma.  




Mwenyekiti wa msafara Twende Butiama Gabriel Landa, alisema kuwa msafara huo una lengo la kumuenzi Baba wa Taifa kwa vitendo kwasababu Mwl. Julius Nyerere alitumia chombo cha baiskeli wakati alipokuwa mwalimu na hata alipoacha uwalimu na kuanza harakati za kupigania uhuru na mambo mbalimbali alitumia baiskeli. Mwalimu Nyerere pia aliwahi kusafiri kwa kuendesha baiskeli kutoka Dar-es-Salaam hadi Arusha, aliongeza.

Msafara huo umewaunganisha watu wa nchi mbalimbali kwa kuonesha Mwalimu Nyerere alikuwa sio mbinafsi bali mpenda umoja. “Wengi wanaotuona barabarani wanahisi haya ni mashindano ila haya sio mashindano bali ni msafara wa kawaida ambao tunaendesha baiskeli kwa mwendo wa upendo ambao ni mwendo wa taratibu” alisema Landa.

Aidha, Landa aliongeza kwa kusema, wameamua kumuenzi kutokana na falsafa yake ya kupinga maadui wa maendeleo kwa kushirikiana na taasisi binafsi kwa kuzisaidia shule mbalimbali ili kupunguza changamoto na adha wanazozipata wanafunzi na walimu wakiwa darasani. “Kupitia wadau mbalimbali tumeweza kukabidhi madawati zaidi 1,000 katika shule zaidi ya 13 hadi kufikia mwaka jana. Lakini tumeweza kupanda miti zaidi ya 50,000 na kuhamasisha watanzania kujali afya zao kupitia programu mbalimbali” aliongeza.




Msafara huo wa waendesha baiskeli ulitokea Dar-es-Salaam tarehe 30 Septemba, 2024 na kufika Dodoma Oktoba Mosi 2024 majira ya jioni. Msafara unajumuisha rika zote kuanzia wazee miaka 60, vijana na watoto wakitokea maeneo mbalimbali ya Tanzania bara na Zanzibar nan chi jirani za Kenya, Burundi, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma