Gari la Darasa Tembezi latoa elimu Mitaa ya Jiji la Dodoma

Na. Asteria Frank, DODOMA

Gari la Darasa Tembezi kutoka Halmashauri ya Jiji Dodoma linalopakia abiria kwa lengo la kuelimisha kuhusu uandikishaji wa orodha ya wapiga kura kuelelea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa linaendelea kuwafikia wananchi wengi katika maeneo mbalimbali ya halmashauri.


Darasa Tembezi linapita kwenye kila kituo likipakia abiria na kuwapa elimu kisha linawashusha katika vituo vyao kwa kuhakikisha wameelewa zoezi la kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura zoezi lililoanza tarehe 11-20 Oktoba, 2024 kuelekea Uchaguzi wa Serikali Mitaa.

Muelimishaji na muhamasishaji wa Darasa Tembezi, Isabella Bruno aliwaeleza abira kuwa kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika tarehe 27 Novemba, 2024 na kusema kuwa mwananchi wanatakiwa kujiandikisha kwenye orodha ya wapiga kura katika vituo vilivyopo katika ofisi za mitaa, shule za msingi na sekondari, zahanati na vituo vya afya, maeneo ya wazi yenye mikusanyiko ya watu na majengo mengine ya taasisi za umma yaliyopo katika mitaa au vitongoji ili aweze kushiriki kuchagua mwenyeki pamoja na wajumbe wa kamati ya utekelezaji.

Alisema kuwa kuna utofauti kati ya kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpiga kura ambalo liliwawezesha wananchi kupata kadi ya kupigia kura mwaka 2025 kwenye kuchagua diwani, mbunge na raisi. Kujiandikisha kwenye orodha ya wapiga kura ni kwaajili ya kupata sifa ya kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na linabeba orodha ya wananchi wanaoishi katika eneo husika pekee.

“Zoezi la kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la mpiga kura haliusiani kabisa na Uchaguzi wa Serikaliza Mitaa. Kwahiyo, ili kupata sifa ya kushiriki Uchaguzi wa Serikari za Mitaa ni lazima ujiandikishe kwenye orodha ya wapiga kura katika mitaa tunayotoka” alisema Bruno.

Aliongeza kuwa kupata sifa ya kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni lazima awe raia wa Tanzania, mwenye umri wa miaka 18 na kuendelea, na mkazi wa mtaa ambao uchaguzi unafanyika. Pia awe na akili timamu na awe amejiandikisha kupiga kura katika mitaa husika na zoezi la kujiandikisha ni la muda mfupi.

Balozi wa kupinga Rushwa, Noela Maginga alisema kuwa ruswa ni kitendo cha kutoa au kupokea kitu chenye thamani bila kufuata taratibu au kwenda kinyume na sheria. Hivyo, kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na hata uchaguzi ujao mwakani vitendo vya rushwa havitakiwi kuchukua nafasi ikiwemo rushwa ya ngono.

“Mimi kama Balozi wa kupinga rushwa napenda kuwakataza msipokee wala msikubali kuchukuwa rushwa na kama unaweza kukutana na tatizo kama hilo unawza kupiga namba 113 kwaajili ya kuripoti ukiwa na ushahidi asanteni na ninawaomba mshiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa” alisema Maginga.

Abiria wa gari la Darasa Tembezi, Aliy Mhagama alisema kuwa amefurahia kupata elimu kuhusu swala zima la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na kupewa utofauti kati ya daftari la kudumu la mpiga kura na orodha ya wapiga kura.

“Mimi kama kijana nawahusia na nina wakumbusha vijana wenzangu kuwa jambo la Serikali za Mitaa ni la zuri sana na limeidhinishwa na katiba ya nchi yetu. Kwahiyo, ni vema sisi sote kushiriki ili tuweze kuchagua viongozi bora na walio sahihi na ambao wanaweza kuja kutuletea mabadiliko. Hivyo, vijana wenzangu tusibaki nyuma twende tukajiandikishe kwenye orodha ya wapiga kura” alisema Mhagama.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma