Ujenzi wa Kituo Kipya cha Afya Chang'ombe kusaidia wananchi zaidi ya 200 kwa siku

Na. John Masanja, CHANG’OMBE

Wananchi wa Kata ya Chang’ombe waishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kupunguza kadhia ya upatikanaji wa huduma za afya kupitia ujenzi wa Kituo kipya cha Afya Chang’ombe.

 

Diwani wa Kata ya Chang’ombe, Bakari Fundikila akifafanua jambo


Akizungumza katika mahojiano maalum na wanahabari, Diwani wa Kata ya Chang’ombe, Bakari Fundikila alisema kuwa ujenzi wa kituo hicho uliogharimu zaidi ya shilingi Milioni 500 umekuwa na msaada mkubwa kwa wakazi wa kata hiyo. Kituo hicho ni msaada pia kwa wananchi wa maeneo ya pembezoni kwakuwa awali walikuwa wanatembea umbali mrefu kutafuta huduma za kiafya.

 

Diwani Fundikila alisema kuwa kwasasa kituo hicho kinaendelea kutoa huduma mbalimbali za kawaida na za kibingwa kwa wananchi. Alisema kuwa kabla ya ujenzi wa kituo hicho huduma hizo walikuwa wakizifuata katika hospitali kubwa zilizo mbali ikiwemo Hospitali ya Mkoa wa Dodoma.

 

“Ukienda kutazama taarifa za wagonjwa, utakuta kwa siku kituo hiki kinahudumia wagonjwa zaidi ya 200. Kwetu sisi ni jambo la kushukuru sana kwa kujengewa kituo hiki cha afya” alisema Diwani Fundikila.

 

Aidha, alizitaja baadhi ya huduma za kibingwa zinazotolewa kituoni hapo kuwa ni matibabu ya meno pamoja na huduma za uzazi kwa wanawake ambazo awali hazikuwepo. Hivyo, alitoa rai kwa wananchi kufika na kupata huduma kituoni hapo.

 

Kwa upande mwingine Diwani Fundikila alimshukuru Rais, wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha, shilingi Milioni 265 katika kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Polisi cha daraja “C” kinachojengwa katika Kata ya Chang’ombe.

 

“Awali, wazo la ujenzi wa kituo hiki cha Polisi kiliibuliwa na wananchi na ndipo walianza kukijenga na baadae tulipoomba fedha serikalini, takapatiwa kiasi cha shilingi Milioni 265 ili kuhakikisha ujenzi huu unakamilika na matengemeo yetu, mpaka ifikapo mwishoni mwa mwaka kitakuwa kimekamilika” alisema Diwani Fundikila.

Akihitimisha mahojiano yake na wanahabari alitoa rai kwa wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anazozifanya katika ujenzi wa miradi na uboreshaji wa huduma mbalimbali kwa kutunza miundombinu hiyo ili itumike kwa muda mrefu.

 

Nae, Gerald Pater, Mkazi wa Kata ya Chang’ombe aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa ujenzi wa kituo cha afya na kusema kuwa atahakikisha anatoa elimu kwa wananchi wenzake kuhusu jitihada hizo. Alisema pia ili kituo hicho kidumu ni wajibu wa kila mwananchi kukitunza.

 

“Kwa upande wangu nafurahia ujenzi huu wa Kituo cha Afya Chang’ombe kwa kuwa hadi sasa kimeturahisishia wananchi kupata huduma za kiafya kwa haraka na wepesi ukilinganisha na hali iliyokuwa awali” alisema Grace Chatanda Mkazi wa Chang’ombe.

 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma