Wanafunzi Dodoma watakiwa kutoa taarifa za ukatili wa kijinsia

Na. Dennis Gondwe, CHAMWINO

WANAFUNZI wa shule za msingi mkoani Dodoma wametakiwa kutoa taarifa kwa Dawati la Jinsia na Watoto pindi watakapofanyiwa ukatili wa kijinsia ili kuwa na jamii isiyo na ukatili wa kijinsia.

Mkaguzi wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma, Theresia Mdendemi akiongea na wanafunzi


Kauli hiyo ilitolewa na Mkaguzi wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma, Theresia Mdendemi, kutoka Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Dodoma alipokuwa akiongea na wanafunzi wa Shule ya Msingi Chamwino katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Insp. Mdendemi alisema “watoto wazuri msisite kutoa taarifa kwa Dawati la Jinsia na Watoto katika Jeshi la Polisi na watu mnaowaamini pindi mnapofanyiwa ukatili wa kijinsia. Hakikisha ndani ya saa 72 mmetoa taarifa kwenye Dawati la Jinsia na Watoto au mtu mnaemwamini ili tuweze kupata Ushahidi. Mtuhumiwa tunatakiwa tumuunganishe kosa alilofanya na ushahidi tutakaopata toka kwenye mwili wako”.

Alisema kuwa mara nyingi ukatili umekuwa ukifanyika kwa watu wa karibu jambo linalofanya mara nyingi matukio hayo kutoripotiwa. “Kwa hiyo tunatoa rai, awe baba au mama, awe shangazi au mjomba, awe mama wakufikia au baba wakufikia, amefanya ukatili toa taarifa mapema ili tuweze kulishughulikia” alisisitiza.

Alisema kuwa kutoa taarifa mapema kutawawezesha kuwaepusha watoto waliofanyiwa ukatili na magonjwa yanayoambuliza. “Unapotoa taarifa mapema unatoa mwanya kwa sisi kuweza kukusaidia wewe usipate magonjwa yanayoambukiza mfano maambukizi ya virusi vyua ukimwi, mimba zisizotarajiwa na magonjwa ya zinaa. Naimani kwa ujumbe huu mtakuwa mpo tayari kushirikiana na dawati la jinsia kwa kutoa taarifa sahihi, hata kama haumfahamu jina aliyekufanyia ukatili ila ukamtaja kwa muonekano kwa mfano alionekana ni mweupe, ana masharubu, anaongea rafuzi flani, huo ndio utoaji taarifa sahihi. Lakini mnapokuwa barabarani mmekuwa mkifanyiwa ukatili, angalia rangi ya gari, muonekano wa gari pia shika namba za gari” alisema Mkaguzi wa Polisi Mdendemi.

Kwa upande wake, Cpl. Edith Siwango kutoka Dawati la Jinsia na Watoto wa Jeshi la Polisi Wilaya ya Dodoma aliwataka wazazi kutenga muda kuzungumza na watoto wao. “Tupo hapa kwa ajili ya kuwalinda watoto wetu. Wazazi mlio hapa nawaomba mtenge muda wa kuzungumza na watoto wenu ili wawe wanaelewa. Kuwachapa watoto siyo suluhisho, kuongea nao na kuwaelimisha ndiyo suluhu. Kumuelekeza mtoto ndiyo suluhu kwa maisha ya sasa. Kama unataka mtoto wako awe msikivu ongea nae, tusiwaachie walimu peke yao, tukiongea nao watatueleza changamoto zao” alisema Cpl. Siwango.

Cpl. Edith Siwango kutoka Dawati la Jinsia na Watoto wa Jeshi la Polisi Wilaya ya Dodoma




 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma