TIMU YA WATUMISHI JIJI LA DODOMA YAIBUKA KIDEDEA KWA KUBEBA VIKOMBE 5 SHIMISEMITA TAIFA

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

TIMU ya Watumishi ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma iliyoshiriki michezo ya Shirikisho la Michezo Serikali za Mitaa (Shimisemita) ilikuwa tishio kwa kushinda michezo yote mpaka fainali na kuzoe vikombe vitano.


Katibu wa Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma, Emma Ernest alipokuwa akisoma taarifa fupi ya michezo ya Shimisemita

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa Timu ya Watumishi Jiji la Dodoma, Emma Ernest alipokuwa akisoma taarifa fupi ya michezo ya Shimisemita ngazi ya taifa mwaka 2023 kwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma katika hafla fupi ya kukabidhi vikombe walivyoshinda katika mashindano ya michezo ya Shimisemita katika ukumbi wa mikutano wa jiji hilo.

Ernest alisema “katika michezo yote timu yetu ilikua ni tishio katika mashindano kwasababu michezo yote tuliyocheza hatukuwahi kufungwa hata mechi moja, tulishinda mechi zote kutoka hatua ya mzunguko mpaka fainali.  Timu ya mpira wa miguu ndiyo iliishia robo fainali kwa kutolewa na timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba kutokana na wachezaji wengi kuwa majeruhi”.

Alisema kuwa katika mashindano hayo halmashauri hiyo iliweza kushiriki michezo yote pamoja na changamoto ya uchache wa wachezaji. “Wachezaji walijituma kwa moyo wote na kuweza kushinda michezo yote na Jiji la Dodoma kuibuka kidedea mshindi wa jumla kwenye michezo ya Shimisemita mwaka 2023 na kuipeperusha bendera ya Jiji la Dodoma ipasavyo. Pamoja na hayo Daktari Bora wa mashindano aliyeokoa maisha ya wachezaji wote alitoka katika halmashauri yetu ambae ni Dr. Baraka F. Edwin” alisema Ernest.

Timu ya watumishi wa Jiji la Dodoma ilishiriki michezo ya mpira wa miguu, mpira wa pete, mpira wa wavu, mpira wa mikono, pooltable, draft, darts, ngoma, karata na riadha. “Ikiwa na jumla ya wachezaji 40, Daktari 2, Kocha 2, Dereva, Timu Meneja, Katibu, Mwenyekiti, Afisa utumishi na Mlezi wa Timu. Tunamshukuru Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kwa juhudi na jitihada alizozionesha kwa wachezaji kwa kuwatia moyo na kuwawezesha kushiriki mashindano tukiwa na afya njema, tabasamu la ushindi lililopelekea kurudi na ushindi mnono huku tukiziangusha Halmashauri 69, tunakupongeza sana mwajiri wetu na tunaimani na wewe uzidi kututia moyo ili bendera ya Jiji la Dodoma ipepee kwa shagwe kwa kila sekta ndani na nje ya nchi yetu” alisema Ernest.

Mashindano ya Shimisemita yalianza tarehe 18-30 Oktoba, 2023 na timu ya watumishi wa Dodoma Jiji iliibuka mshindi wa jumla kwa kunyakua makombe matano, wanawake nafasi ya mshindi wa kwanza katika mpira wa pete, wavu, na mikono, huku wanaume wakishika nafasi ya pili mpira wa mikono na medali nne (mbili pooltable, moja draft na moja kurusha tufe) huku daktari bora wa mashindano aliyeokoa maisha ya wachezaji wote alitoka Jiji la Dodoma.



MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma