MEYA AKEMEA UZALISHAJI MIGOGO JIJI LA DODOMA

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MSTAHIKI Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe amekemea tabia ya uzalishaji migogoro ya ardhi na kusema inarudisha nyuma maendeleo ya halmashauri.

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe


Prof. Mwamfupe alisema hayo alipokuwa akitoa muhtasari wa hoja zilizoibuliwa katika Mkutano wa Chama wa Mwaka wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Alisema “tunakemea watu wote wanaojihusisha na kuzalisha migogoro katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Na katika hili Mkurugenzi wa Jiji, watumishi wachukue nafasi zao na kwamba tutasimama kuhakikisha hatuibui migogoro mingine ya ardhi. Yapo maeneo madiwani wake wametuhumiwa kuhusika na migogoro ya ardhi. Rai ya kikao ilikuwa hawa wajitokeze tufanye nao mkutano wa Pamoja Meya, Mkurugenzi wa Jiji na Mkuu wa Divisheni ya Uendelezaji Makao Makuu. Mkutano huo ni wa kuwataka kutoa picha ya muelekeo wao na jinsi wanavyoifahamu hiyo migogoro na wengine watatupa muelekeo zaidi juu ya migogoro hiyo”.

Eneo lingine la msisitizo alilitaja kuwa ni kufungua barabara za mitaa ili ziweze kupitika kabla ya msimu wa mvua.

Mstahiki Meya alisema kuwa eneo lingine lililosisitizwa ni kusimamia mapato ya halmashauri. “Kuhakikisha tunaenda kusimamia mapato ya halmashauri kikamilifu ili tuweze kukamilisha miradi tuliyojipangia. Pia miradi viporo katika kata zote ikamilike kwa mujibu wa bajeti” alisema Prof. Mwamfupe.

Msisitizo mwingine ni kupunguza upungufu wa wafanyakazi wa kada za elimu na afya wa maeneo ya pembezoni na wananchi waliotwaliwa maeneo yao waweze kulipwa fidia. “Katika hili tunatambua baadhi ya malipo yanatoka serikali kuu, lakini yale malipo yanayotoka halmashauri yalipwe” alisema Prof. Mwamfupe.

MWISHO.

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma