JIJI LA DODOMA LAISHUKURU SERIKALI FEDHA ZA MAENDELEO

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imetoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha 2022/2023 jambo lililosogeza huduma za kijamii na maendeleo karibu na wananchi.

Mkuu wa Divisheni ya Mipango na Uratibu wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Francis Kaunda


Shukrani hizo zilitolewa na Mkuu wa Divisheni ya Mipango na Uratibu wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Francis Kaunda alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi na uwajibikaji wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kipindi cha mwaka 2022/2023 katika Mkutano wa Mwaka wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa jiji hilo.

Kaunda alisema kuwa katika mwaka wa fedha ulioisha Halmashauri ya Jiji la Dodoma iliweza kutekeleza shughuli mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa ufanisi. “Kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma tunapenda kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa awamu ya sita, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo amekuwa akitoa fedha nyingi za utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Mheshimiwa Rais amekuwa akitoa fedha nyingi kwa stahiki mbalimbali za watumishi wa umma na mishahara kutolewa kwa wakati. Hivyo, kufanya utendaji kazi kwa wataalamu wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kutekeleza majukumu yao kama ilivyopangwa” alisema Kaunda.

Alisema kuwa halmashauri pia imekuwa ikipokea fedha nje ya bajeti zinazosaidia uboreshaji wa huduma za kijamii. “Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia tukipata fedha nje ya bajeti zaidi ya bilioni 4.9 na fedha hizo zimeelekezwa katika kuhakikisha huduma bora na kwa wakati zinaweza kutolewa kwa wananchi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma” aliongeza Kaunda.

 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma