ASMA KARAMA ACHAGULIWA NAIBU MEYA JIJI LA DODOMA

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

ASMA Said Karama amechaguliwa kwa asilimia 100 kuwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika Mkutano wa Mwaka wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika ukumbi wa halmashauri.

Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Asma Said Karama


Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, Mwenyekiti wa Uchaguzi wa Naibu Meya, Sakina Mbugi alisema “Mheshimiwa Asma Said Karama amepata kura 55 sawa na asilimia 100 ya kura zote zilizopigwa na wajumbe. Kwa mamlaka niliyopewa ninamtangaza Mheshimiwa Asma Said Karama kuwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma”.

Akitoa neno la shukrani Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Asma Karama alisema alimshukuru Mungu kwa baraka zake. “Napenda kukishukuru chama changu cha Mapinduzi kwa kuniruhusu kuingia kinyang’anyiro hiki. Kipekee zaidi napenda kuwashukuru madiwani kwa kuniamini na kunituma ili niwatumikie, tufanye kazi pamoja na kumsaidia Mstahiki Meya na kuwaletea maendeleo wana Dodoma. Kipekee zaidi nashukuru kuwa mwanamke pekee niliyewahi kuingia kuongoza unaibu Meya katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma” alisema Karama.

Vilevile, alimshukuru Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwatia moyo na nguvu wanawake kugombea nafasi za uongozi. “Nipo pamoja na ninyi kufanya kazi zilizotukuka ili kuwatumikia wananchi waliotuchagua. Mapungufu yangu mimi kama mwanadamu na ninyi kama wanadamu twende tukikosoana na tukirekebishana ili tufikie lengo kwa umoja wetu. Nawaazima masikio yangu na moyo wangu wote kuwasikiliza na mimi mniazime masikio yenu tusikilizane ili tuweze kutumikia Halmashauri ya Jiji la Dodoma” alisema Karama kwa upole.

Nae Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, John Kayombo alimhakikishia Naibu Meya ushirikiano. “Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi kwa niaba ya wataalam tunakuhakikishia tutakupa ushirikiano wa kutosha ili yale maelekezo utakayopewa na Mstahiki Meya uyatekeleze kwa usahihi” alisema Kayombo.

Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, John Kayombo


MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma