CHEMS YAJIKITA KUZALISHA MADUME BORA YA MBUZI DODOMA

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

CHEMS farm imedhamiria kuzalisha madume bora ya Mbuzi aina ya Boha ili kuwasaidia wafugaji kuboresha mifugo yao ya asili katika kanda ya kati.

Mfugaji wa Mbuzi kutoka Chems farm, Vendelin Lyakurwa


Kauli hiyo ilitolewa na Mfugaji wa Mbuzi kutoka Chems farm, Vendelin Lyakurwa alipokuwa akielezea ufugaji wa Mbuzi katika Banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwenye maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni jijini hapa.

Lyakurwa alisema “lengo la kuzalisha na kuwatunza hawa Mbuzi aina ya Boha ni kuuza madume kwa wenzetu ili waweze kuboresha mifugo yao ya asili. Ukiwa na dume moja kwenye boma unaweza kukusaidia kupata mbegu ambayo wanakua haraka na bei yao ni nzuri na nyama yao ni tamu. Mbuzi hawa ni wa nyama na wanazaa mapacha ukiwalisha vizuri wanazaa pacha watatu mpaka wanne. Wanakuwa haraka wanasoko mpaka uarabuni wanawahitaji hawa Mbuzi. Ni Mbuzi ambao ‘wanaadapt’ mazingira mbalimbali”.

Alisema kuwa madume wakitumika kwa Mbuzi wa kienyeji wanachukua uzao wa baba. “Wanakuwa haraka na wanakuwa na nyama nyingi na uzito unakuwa mkubwa ingawa wanakuwa chotara. Ni Mbuzi wazuri na wanakuwa haraka kwa miezi mitatu kama unamtunza vizuri anakuwa na uzito wa kilo 22-36 anapoachishwa kunyonya” alisema Mkulima Lyakurwa.

Alisema kuwa ameuza mbegu ya madume hao maeneo mbalimbali. “Nimeuza Kigoma, Kagera, Morogoro, Pwani, Zanzibar, Mtwara na Ruvuma. Ili wakuwe vizuri wanatakiwa kula vizuri. Ukiwaoteshea majani, uwape na chakula cha ziada kama pumba wanakuwa haraka na mafanikio yake ni makubwa na kukuletea utajiri wa hali ya juu” alisema Lyakurwa.

Alisema kuwa Mbuzi hao wana bei nzuri sokoni. “Nyama yake ni nzuri na inafika shilingi 20,000 sokoni. Akiwa na kilo 100 ukimchinja unapata nyama kilo 55 maana yake unaweza kumuuza hadi shilingi 1,200,000. Ni wazuri kwa biashara kwa sababu mama zao wanazaa mapacha kwa miaka miwili wanakuzalia mara tatu” alisema Lyakurwa.

Maonesho ya shughuli za wakulima Nanenane mwaka 2023 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na wanawake ni msingi imara wa mifumo endelevu ya chakula”.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Global Affairs Canada yafurahishwa na utekelezaji wa Mradi wa AHADI katika Kata ya Chamwino

Umeme wa REA chachu ya viwanda vidogo vidogo Kata ya Ipala

Kata ya Ipala ipo mstari wa mbele katika Michezo