Elimu ya Lishe inapatikana Banda la Nanenane Jiji la Dodoma

Na. Mwanaidi Masudi, DODOMA

Mjasiriamali kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Agnes Kinyaii, ametoa elimu ya kina kuhusu umuhimu wa lishe bora kwa wananchi waliojitokeza kwenye maonesho ya Nanenane kitaifa yanayofanyika jijini Dodoma.

 

Akizungumza katika banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Kinyaii aliwasisitiza wananchi kuzingatia ulaji wa lishe bora kama utumiaji wa viazi vya ‘bitreat’ vinavyosaidia mambo makuu manne kuongeza damu, kukinga maradhi ya damu na afya ya mifupa ya meno.

 

Aliendelea kuelezea kuwa upo unga wa lishe uliotengenezwa katika utaratibu ambao unampatia mtu virutubisho zaidi ya kushiba. “Kwamba tumechanganya vitu vikuu vinne, tumeweka mahindi lishe na viazi lishe, mbegu nyeusi za maboga. Lakini pia tumeweka ‘Almond’ na ngano isiyo kobolewa. Kwahiyo, huu unga anatumia mtoto mdogo anayeanza kula mpaka mzee na ukila hauwezi kukuzidi nguvu kwasababu hatujazidisha wanga. Tumeweka vitu viwili vinavyotoa wanga yaani viazi na mahindi lishe ambayo yana viwango vikubwa vya Vitamin A zaidi hata ya wanga. Kwahiyo, mtu anayetumia huu unga anakuwa na Vitamin A pamoja na wanga ndio maana tunasema hiki ni chakula anatumia mtoto mpaka mtu mzima” alieleza Kinyaii.

 

Wakati huohuo, alielezea zao la mwani kuwa ni zao la baharini ambalo hupatikana maeneo ya fukwe za bahari kama Tanga, Bagamoyo, Dar es Salaam na Pwani kwa sababu linapenda maji ya chumvi. Ni moja ya zao lenye virutubisho vingi vinavyohitajika kwenye mwili wa binadamu wenye madini 72.

 

Vilevile, aliendelea kuonesha wananchi bidhaa mbalimbali wanazotengeneza za lishe hususani unga wa lishe ambao unawasaidia mama wanaonyonyesha kuongeza kiwango cha maziwa. “Uji huu tumeweka mbegu nyeusi za maboga, mbegu hizo zimetengenezwa mahususi kwa ajili ya kuchochea utengenezaji wa maziwa kwa kina mama. Kwahiyo, yule anayenyonyesha akitumia huu uji anakuwa anapata maziwa mengi sana, wamama wengi wanapata changamoto za kunyonyesha watoto wao kwa sababu unakuta akishamnyonyesha mtoto wake anakaukiwa maziwa. Lengo ni kuhakikisha hakuna mtoto ambaye anaanzishwa kula kabla hajafikisha miezi sita, mama anayenyonyesha akitumia huu uji wetu anakuwa anapata maziwa mengi na ya uhakika wa kumnyonyesha mtoto wake miezi sita mfululizo bila kumpa chakula chochote. Ninawasihi sana kina mama wanaonyonyesha watoto walioko katika Jiji la Dodoma wafike katika banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma waweze kujipatia uji huu, tunasema mtoto akinyonya maziwa ya mama anakuwa na akili” alisema Kinyaii.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo