Kura Yako Maendeleo ya Mtaa

Na. Coletha Charles, DODOMA

Timu hamasa ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, imeendelea na zoezi la kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika maeneo mbalimbali ya halmashauri hiyo.

 



Zoezi hilo lilifanyika katika eneo la Soko la wazi la Machinga hadi Ihumwa kwa lengo la kuwakumbusha na kuwasisitiza wananchi umuhimu wa kupiga kura kwasababu ni msingi mzuri wa kuleta maendeleo katika mitaa yao.

 

Muelimishaji wa katika gari maalum lijulikanalo kama darasa tembezi, Isabella Bruno alisema kuwa kupitia Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Dodoma kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, wametoa gari la darasa tembezi kwa lengo la kuhamasisha wananchi kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka huu.

 

Alisema kuwa wananchi wanatakiwa kuchagua viongozi wenye sifa kwa kusikiliza sera zao kipindi ambacho kampeni zitakapoanza tarehe 20 Novemba, 2024 na kuangalia kiongozi wa kuwaongoza kwa muda wa miaka mitano ya uongozi.

 

“Tunafanya hivi kukupa uelewa wewe mwananchi na kukukumbusha kuwa ni wajibu wako kupiga kura, kama tunavyofahamu wananchi wengi tumekuwa na kasumba ya kutokushiriki masuala ya uchaguzi kwa sababu mbalimbali na wengine wanakuwa hawaoni umuhimu wa kushiriki” alisema Bruno.

 

Kuhusu suala la rushwa, wananchi wametakiwa kutojishughulisha na kutoa au kupokea rushwa kwa lengo la kumchangua kiongozi asiye sahihi kwasababu uchanguzi huu ni wa amani na wakuleta tija katika nyanja tofauti tofauti.

 

Uchaguzi huu unatarajiwa kufanyika tarehe 27 Novemba, 2024 na kila mwananchi mwenye sifa na vigezo vya kushiriki atatakiwa kupiga kura akiwa ni mtanzania halisi, mwenye umri kuanzia miaka 18 na kuendelea, mwenye akili timamu, mkazi wa mtaa husika na awe amejiandikisha kwenye orodha ya daftari la wapiga kura.

MWISHO

 

 

 

Comments

Popular Posts

Osterbay Dodoma wajitokeza usafi wa mazingira

Usafi wa Mazingira Kipaumbele Kata ya Chamwino

Wananchi wa Kata ya Mtumba wanufaika na Mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri