Jiji la Dodoma lasaini mkataba ujenzi wa barabara ya lami kwenda Hospitali ya Jiji

Na. John Malima, DODOMA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imesaini mkataba wa makubaliano ya ujenzi wa barabara kutoka Hospitali ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma hadi barabara kuu ya Singida yenye urefu wa Kilomita 1.6 kwa kiwango cha lami.


Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe (kustoto) na Mkurugenzi wa Jiji, Dkt. Frederick Sagamiko wakisaini mkataba wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami


Mkataba huo ulisainiwa tarehe 20 Novemba, 2024 katika Ofisi ya Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma baina ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma na Kampuni ya ujenzi ya Kings Builders Limited ukiwa na thamani ya shilingi 2,431,050,561.63 (Bilioni Mbili na Milioni Mia Nne Thelathini na Moja Laki Tano na Mia Tatu Sitini na Moja na senti Sitini na Tatu).

Katika zoezi la kusaini mkataba huo Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe alimshukuru Mkandarasi kwa kuunga juhudi za serikali na alimtaka kufanya kazi kwa viwango vinavyotakiwa. “Kwanza nawapongeza sana, mmetimiza adhma ya serikali kwamba katika miradi iliyo mingi tunasisitiza sekta binafsi, lakini tungependa msiwe vikwazo katika utekelezaji wa miradi yenu kwasababu Dodoma ni makao makuu ya nchi. Kama utendaji kazi wenu utakuwa wa viwango, mtakua mnaunga mkono juhudi za serikali. Kwahiyo, lazima tuhakikishe ubora wa miundombinu ili kuifanya sekta ya afya istawi zaidi” alisema Prof. Mwamfupe.

Kutokana na changamoto mbalimbali za wakandarasi kutokumaliza miradi yao kwa wakati, Mstahiki Meya alimtaka mkandarasi kutokuwa kero katika utekelezaji wa mradi huo kwa visingizio mbalimbali. “Tungependa ninyi msije mkawa kero, kwa maana kwamba kazi zenu haziishi kwa visingizio visivyoisha kama vifaa, bei na vingine vingi, hatutegemei kujuta kutokana na kazi hii kwasababu ubora wa kazi hii ni namna ya kuomba kazi nyingine tena” alisisitiza Prof. Mwamfupe.


Mkandarasi Eng. Joseph Tarimo (kulia) akisaini mkataba wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami


Kwa upande wake, Mkandarasi wa Kampuni ya Ujenzi ya Kings Builders Limited, Mhandisi Joseph Tarimo, aliyesaini mkataba huo amesema watajitahidi kufanya kazi kwa muda walioahidi wakizingatia ubora katika mradi huo.

“Sisi kama kampuni, tunaunga mkono yale aliyosema Mstahiki Meya, kampuni tutafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kuwa tunakamilisha kazi ndani ya muda wa mwaka mmoja lakini ni mategemeo yetu tutafanya kazi hii kwa pungufu ya muda uliopo katika mkataba wetu” alisema” Mhandisi Tarimo.

Ukarabati wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami utakuwa na manufaa kwa wakazi wote wa Jiji la Dodoma kwasababu itarahisisha upatikanaji wa huduma ya Afya na shughuli za uchukuzi.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma