Jiji la Dodoma latoa Kilo 790 za sukari kwa shule 150

Na. Faraja Mbise, DODOMA

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imetoa kilo 790 za sukari kwa ajili ya walimu wa shule za msingi na sekondari ili kuwawezesha kupata uhakika wa chai wanapokuwa shuleni ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais wa Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Dodoma mjini za kuhakikisha nishati safi ya kupikia inatumika katika taasisi mbalimbali.




Kilo hizo zilitolewa na Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhili Chibago wakati wa hafla ya ugawaji mitungi ya gesi na majiko 1,000 kwa shule, zahanati, vituo vya afya, vituo vya watoto yatima na mama na baba lishe tukio lililofanyika katika uwanja wa Nyerere square jijini Dodoma.

Naibu Meya Chibago alisema kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma imechangia kilo 790 za sukari kwa shule za msingi na sekondari 150. Shule za msingi zilizopewa sukari hiyo ni 104 na shule za sekondari ni 46 ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais wa Tanzania na mbunge wa jimbo la Dodoma mjini, aliongeza.

Akiongelea zoezi la utoaji wa majiko na mitungi 1,000 ya gesi kwa taasisi mbalimbali, alisema kuwa ni jambo la kizalendo. “Kwa niaba ya wananchi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma na kwa moyo wa unyenyekevu sana tunataka kukushukuru sana kwa moyo wako, bila kusukumwa na yeyote kwa nia yako ya dhati ya kulipenda Jimbo lako la Dodoma mjini.... Sisi Halmashauri ya Jiji la Dodoma tumepokea kwa mikono miwili maoni ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutamani watanzania wote tuondokane na matumizi ya kuni lakini pia tutumie sasa nishati mbadala” alisema Chibago.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Dodoma Mlimani, Mwl. Jenifa Mhavile aliishukuru Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa ugawaji wa sukari na mitungi ya gesi katika shule. Alisema kuwa itawasaidia kuokoa muda wakati wa kupika chai  ofisini na pia watatoa elimu kuhusu utumiaji wa nishati safi na   kuhamasisha utumiaji wa nishati safi ya kupikia katika vikao vya wanafunzi na wazazi. “Kutokana na kuwa tupo katika kampeni ya kupinga matumizi ya nishati chafu tutatumia elimu hii kuhamasisha juu ya matumizi sahihi ya gesi. Tutahakikisha kuwa kila mmoja anakuwa balozi katika masuala ya matumizi ya gesi” alisema Mwl. Mhavile.




Hafla ya ugawaji wa mitungi ya gesi na majiko 1,000 kwa shule, zahanati, vituo vya afya, vutuo vya makao ya watoto na mama na baba lishe ni kuunga mkono jitihada za Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia. Halfa hiyo ni ya tatu kwa Mbunge Anthony Mavunde, ambapo awamu ya kwanza nay a pili alitoa jumla ya majiko 1,500 kwa lengo la kupunguza matumizi ya nishati chafu ya kupikia ambayo ina athari kubwa katika mazingira na kupelekea vifo vya watu wengi nchini.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma