DC Shekimweri ahamasisha wananchi kushiriki uboreshaji daftari la wapiga kura

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri amewataka wananchi wa Jiji la Dodoma kujitokeza katika zoezi la kujiandikisha katika kuboresha daftari la kudumu la wapiga kura na kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika tarehe 27 Novemba, 2024.



Alhaj Shekimweri, aliyasema hayo katika Bonanza la wadau lililofanyika katika viwanja vya Sheli Complex iliyopo Mtaa wa Mailimbili, Kata ya Chamwino jijini Dodoma.

Akizungumza na wananchi pamoja na wadau mbalimbali Alhaj Shekimweri alisema “Kwa Jiji la Dodoma ukizingatia takwimu za Sensa ya mwaka 2012 ilikuwa na wakazi karibu Laki tano kasoro, Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 lilikuwa na wakazi 798,000 na ukizingatia ongezeko karibu la 3% kwa mwaka tunakaribia kufikia Milioni Moja kasoro. Takwimu zinaonesha idadi ya wapiga kura kwenye wilaya yetu ni 502,000”.

Aidha, aliongeza kwa kusema kuwa utoaji wa elimu kuhusu uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura utakuwa ni endelevu na watatumia njia mbalimbali kufikisha ujumbe kwa jamii. Njia hizo alizitaja kuwa ni kutumia bonanza, ushirikishwaji wa wasanii, matumizi ya vyombo vya habari, uchapishaji wa mabango na uhamasishaji wa ana kwa ana.

Bonanza hilo lililoongozwa na kaulimbiu isemamayo “Serikali za Mitaa, sauti ya wananchi, jitokeze kushiriki uchaguzi” lilipambwa na burudani na michezo kama vile mpira wa miguu, kuvuta kamba, kukuna nazi, mchezo wa bao, rede, pamoja na muziki na maigizo kutoka kwa wadau mbalimbali kama Taasisi ya Mama Samia, kikundi cha muziki wa asili (Hiari ya Moyo) na umoja wa wasanii wanawake Dodoma (UWAWADO).

MWISHO

 

 

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma