Timu ya Veterani kutoka Zanzibar yaibuka mshindi katika Bonanza Dodoma

Na. Valeria Adam, DODOMA

Timu ya mpira wa miguu ya Veterani kutoka Chuo cha Mafunzo Zanzibar imefanikiwa kuibuka mshindi katika Bonanza la mpira wa miguu lililofanyika katika uwanja wa Magereza jijini Dodoma na kupewa kombe.

Mkuu wa Gereza kuu la Isanga, Zephania Neligwa (kulia) akimkabidhi kombe kepteni wa timu ya mpira wa miguu ya Veterani kutoka Chuo cha Mafunzo Zanzibar


Bonanza hilo lilifanyika tarehe 24 Agosti, 2024 kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na uhusiano kati ya Tanzania Bara na Tanzania Visiwani na kuleta burudani kwa mashabiki.

Katika mchezo wa fainali, timu ya Veterani kutoka Chuo cha Mafunzo Zanzibar ilionesha kiwango cha juu, hasa katika eneo la ulinzi ambapo waliweza kuzuia mashambulizi mengi ya wapinzani wao.

Mchezaji wa timu ya Veterani kutoka Chuo cha Mafunzo Zanzibar, Haji Ramadhani alisema kuwa ushindi wao ulitokana na juhudi za pamoja na umakini wa kila mchezaji, huku wakionesha nidhamu ya hali ya juu ndani na nje ya uwanja. “Bonanza limekuwa zuri, kuanzia mwanzo mpaka hatua hii ya kumalizia katika mchezo wa fainali. Kusema kweli mechi zote zilikuwa na ushindani na hili bonanza ni la kihistoria katika Magereza haya”.

“Siri ya ushindi ni kujiandaa vizuri kwa ujumla na tulikuwa tunafanya mazoezi takribani kila wiki pia tulikuja huku kushindana na tunamshukuru Mungu katujalia tumepata ubingwa huu”, alisema Ramadhan.

Kwa upande wa Timu ya Magereza Veterani Makao Makuu ilishindwa katika bonanza hilo walilokabiliana na timu ya Veterani kutoka Zanzibar. Mchezo ulikuwa na ushindani mkubwa, ukionesha tofauti ya maandalizi kati ya timu hizo na Veterani kutoka Zanzibar wakionekana kuwa na uzoefu zaidi.

Akizungumzia matokeo hayo, Emmanuel Sahani, mchezaji wa timu ya Magereza Veterani Makao Makuu, alisema kutokana na ukosefu wa uzoefu kwa timu hiyo na kukosa maandalizi ya kutosha ni moja ya sababu ya timu yao kushindwa. "Wenzetu wako vizuri, walijipanga muda mrefu tofauti na sisi kwa sababu ndio tumeanza, lakini tunashukuru kwa kupata nafasi hii kushiriki na tunaamini kuwa mechi zitakazo kuja mbeleni tutakuwa vizuri zaidi", alisema Sahani.




Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza kuu la Isanga, Zephania Neligwa alisema kuwa michezo hiyo itakuwa chachu ya maendeleo na ushirikiano kati ya Tanzania Bara na Tanzania Visiwani. Pia alimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Wilaya ya Dodoma kwa kuonesha ushirikiano kuanzia mwanzo wa ziara mpaka mwisho wa ziara.

“Mchezo huu umekuwa ni mzuri, mchezo ambao umetuunganisha sisi Tanzania Bara na Tanzania Visiwani na hii itazidi kuweka historia nzuri kati ya Jeshi la Mafunzo la Tanzania Bara na Visiwani".

"Namshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Wilaya ya Dodoma kwa namna ambayo ameshiriki nasi katika tukio hili muhimu, ametuwezesha kuweza kutembelea sehemu mbalimbali za Dodoma", Neligwa alihitimisha.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma