Pikipiki zaendelea kuchangia vifo ajali za barabarani

Na. Anna Stanley, DODOMA

SERIKALI imeeleza kuwa vyanzo vya ajali zinazosababishwa na pikipiki zimeendelea kuchangia vifo ya watu wengi wakati mwaka 2023 zikisababisha vifo wa watu 376 na kupoteza nguvu kazi ya taifa wakati wengine wakiachwa na ulemavu wa kudumu.




Kauli hiyo ilitolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani Kitaifa na miaka 50 ya Baraza la Usalama Barabarani yaliofanyika katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Dkt. Mpango alisema "ndugu wananchi na waheshimiwa viongozi, Pikipiki ni miongoni mwa vyombo vya moto vinavyotoa huduma ya usafiri na usafirishaji wa mizigo na abiria mijini na vijijini, ajali zinazohusu pikipiki zimekuwa nyingi mno zinaongezeka mwaka hadi mwaka kwa mfano katika kipindi cha mwezi Januari mpaka Desemba mwaka jana 2023, kulikuwa kuna jumla ya matukio 435 ya ajali za pikipiki yalioripotiwa katika kipindi hicho, idadi ya vifo vilivyotokana na ajali za barabarani zinazohusisha pikipiki ilikuwa 376 ikilinganishwa na vifo 332 vilivyoripotiwa mwaka 2022".

Aidha, aliwahimiza madereva wa pikipiki kusimamia sheria, hususani uvaaji wa kofia ngumu, kutobeba abiria wengi katika pikipiki moja na umiliki wa wa leseni halali ya udereva pamoja na bima ya chombo cha moto. "Katika kundi hili la ajali za pikipiki hatuna budi kuendelea kusimamia sheria na hususani katika uvaaji wa kofia ngumu, kutobeba abiria wengi katika pikipiki moja na umiliki wa leseni halali ya udereva pamoja na bima ya chombo cha moto. Napenda kutumia nafasi hii kuwasihi sana vijana wangu wa Bodaboda wajiunge na shirikisho lao lakini pia wakate bima ya vyombo vyao vya moto wanavyotumia" alisema Mpango.

Akiongelea vyanzo vya ajali za barabarani, alisema kuwa makosa ya kibinadamu ni chanzo kikubwa. “Makosa ya kibinadamu ndio chanzo kikubwa cha ajali Barabarani, kwahiyo, tunawajibika kuongeza nguvu katika kudhibiti vihatarishi, kuzuia mwendo kasi wa vyombo vya moto, kutovaa kofia ngumu, kutofunga mikanda ya usalama katika magari, ukosefu wa vifaa vya usalama vya kuwalinda watoto wadogo wanapokuwa ndani ya magari" alisema Dkt. Mpango.

Kuhusu madhara yatokanayo na ajali za barabarani alisema kuwa zimekuwa zikisababisha vifo kwa watuvna kupoteza nguvu kazi ya taifa. "Taita letu linapoteza nguvu kazi kubwa kutokana na ajali za barabarani. Takwimu hazipendezi kabisa, mwaka jana 2023 kulikuwa na kesi za ajali 1,647. Aidha, waliopata ajali barabarani walikuwa 2,716 na inakadiriwa kwamba kama hatua madhubuti hazitachukuliwa kukabiliana na hali hii, ajali mbaya za barabarani zitakuwa ndio chanzo kikubwa cha vifo itakapofika mwaka 2030" alisema Dkt. Mpango.



Makamu wa Rais, alilitaka Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani na wadau katika kutokomeza na kuzuia ajali barabarani kuzingatia mambo kadhaa. "Jambo la kwanza ni kuhusu ukaguzi makini na endelevu wa magari na ufanyike kwa mwaka mzima badala ya kusubiri hadi kwenye wiki ya Usalama Barabarani Kitaifa, hasa mabasi yanatakiwa yakaguliwe hata mara nne kwa mwaka. Jambo la pili ni udhibiti wa magari yanayobeba wanafunzi, magari mengi yanayobeba wanafunzi shuleni yana hali mbaya ambayo inatishia usalama wa wanafunzi na madereva wenyewe. Aidha, baadhi ya madereva wa magari hayo wanaonekana kukosa weledi na uadilifu na kusababisha madhara mbalimbali zikiwemo ajali mbaya, kwa mfano halisi ni ile ajali iliyotokea kule Arusha tarehe 12 Aprili 2024 na kusababisha watanzania kuondokewa na vifo vya watoto saba" aliongeza Dkt. Mpango kwa uchungu.

Kadhalika, alivitaka vyombo vya habari kuwa na vipindi ambavyo vinatoa elimu ya Usalama Barabarani kwa umma ili kudhibiti tatizo hili kubwa la ajali barabarani. "Katika hatua hii nina ombi maalumu kwa vyombo vya Habari. Nimefurahi pale TBC wao wana kipindi mara moja kwa wiki kuelimisha umma kuhusu usalama barabarani. Ninaomba na vyombo vingine kuiga mfano huu kuelimisha jamii kupitia redio, televisheni, machapisho mbalimbali, maonesho, sanaa na muziki, mikutano ya hadhara na hata mitandao ya kijamii, lakini pia Jeshi la Polisi nawaomba sana muendeleze kutoa elimu ya usalama barabarani shuleni" alisisitiza Dkt. Mpango.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Barabarani Mkoa wa Dodoma, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ramadhan Ng'anzi ambaye ni Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani aliwahimiza wamiliki wa vyombo vya moto kupeleka magari yao katika ofisi za usalama barabarani mkoa na wilaya kwa ajili ya kukaguliwa kuwa vyombo hivyo vinafaa kwa kutumia barabara ya umma. “Kila chombo cha moto lazima kikaguliwe na baada ya ukaguzi kama kitaonekana kinafaa kwa kutumia barabarani kitapewa 'certificate' maalumu ambacho kinaitwa Stika ya Usalama Barabarani, hii ni 'Certificate' kwamba hili gari limekaguluwa na linafaa kutumia barabara ya umma. Kwahiyo, baada ya maadhimisho haya tutaanza sasa kukamata magari ambayo hayana stika. Kwahiyo, ni muhimu wamiliki wote wa vyombo vya moto waende katika Ofisi za RTO au DTO" alisema DCP Ng'anzi.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma