Mikakati ya Usalama Barabarani inalenga kudhibiti ajali

Na. Flora Nadoo, DODOMA

Mweyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Daniel Sillo ameitaja mikakati ya usalama barabarani kuwa inalenga kudhibiti madereva walevi, wazembe na wanaoendesha kasi Pamoja na mambo mengine.




Alizungumza hayo tarehe 26 Agosti, 2024 katika uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa Wiki ya nenda kwa Usalama Barabarani na Miaka 50 ya Baraza la Taifa la Usalama Barabarani.

Sillo aliwataka madereva na wananchi wawe waangalifu na vyombo vya moto pamoja na sheria za barabarani ili kuepuka ajali za barabarani zisizo za lazima. “Mkakati wa Usalama Barabarani unalenga maeneo yafuatayo uthibiti wa madereva walevi na wanaoendesha kwa uzembe, uthibiti wa mwendokasi kwa madereva, kuwashirikisha wamiliki wa vyombo vya moto katika dhana ya uwajibikaji. Hii ni pamoja na kuhakikisha kunakuwa na madereva wenza kwa mabasi ya masafa marefu. Vilevile, kuthibiti uendeshaji wa magari bila sifa au kutokuwa na leseni za udereva na kutokuwa na bima. Pia udhibiti wa wa usafirishaji wa abiria kwa kutumia magari madogo yenye muundo wa taili moja nyuma kwa mfano Noah na Probox.

“Mkakati huu umedhamirua kudhibiti ajali za pikipiki za magurudumu mawili kama bodaboda na magurudumu matatu. Pia kuhakikisha abiria wanafunga mikanda wanapotumia vyombo vya usafiri. Vilevile, kuyatambua na kuyadhibiti maeneo tete na hatarishi kwa ajali za barabarani, pia kutumia kwa mfumo wa kuweka alama kwenye leseni za madereva ili kuondoa madereva wanaoathiri kwa kukiuka sheria. Hata hivyo, suala la kurekebishwa kwa sheria za barabarani ili ziendane na wakati na zitiliwe maanani namna ya udhibiti wa wimbi la ajali za barabarani pamoja na matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa sheria" alisema Sillo.

Akiongelea umuhimu wa kaulimbiu ya maadhimisho hayo, alisema kuwa inalenga kuwakumbusha watumiaji wa barabara uwajibikaji. Alisema kuwa lengo la kaulimbiu isemayo “Endesha salama, ufike salama” ni kuwakumbusha watumia barabara hususani madereva wa vyombo vya moto na vyombo visivyo vya moto kuzingatia sheria na kanuni za barabarani ili kuwafikisha salama wananchi katika shughuli za uzalishaji mali na kuepusha ajali barabarani zinazogharimu maisha ya wananchi.




Hata hivyo, pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na serikali ya kuboresha miundombinu ya barabara bado kuna tatizo kubwa la madereva wa magari, madereva wa pikipiki na wapanda pikipiki kutojali sheria na kanuni za usalama barabarani. Chanzo kikubwa kinachochangia ajali barabarani ni makosa ya binadamu, ubovu wa vyombo vya moto 12%, mazingira ya barabara 8% na mengineyo kama moto, hali ya hewa na kadhalika, aliongeza.

Akimkaribisha Makamu wa Rais, kuzindua mkakati wa kitaifa wa usalama barabarani, alisema kuwa baada ya miezi sita tangu kuzindua kwa kwa mkakati huo baraza litafanya tathmini kuona maendeleo yatakayopatikana kupitia mkakati huo.

Nae Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango alisema umuhimu wa maadhimisho haya ni kukumbushana juu ya umuhimu wa kutambua na kuthamini usalama wa watu. Alisema kuwa usalama wa watu na usalama wa vyombo vinavyotumia barabara pamoja na miundombinu ya usafiri ni muhimu kulindwa. “Imethibitika kuwa takribani 76% ya ajali nchini kwa maelezo ya IGP hapa zinazosababishwa na makosa ya kibinadamu ambayo yanajumuisha uendeshaji hatari, uzembe wa madereva wa magari au waendesha pikipiki, uzembe wa abiria pia waendao kwa mguu kutokuwa makini wanapovuka barabara” alisema Dkt. Mpango.

MWISHO

 

 


Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma