Kata ya Zuzu yajivunia mafanikio ya utekelezaji miradi ya maendeleo

Na. Valeria Adam, DODOMA

SERIKALI yapongezwa kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha maisha ya wananchi wa Kata ya Zuzu ikiwa na matokeo chanya.




Diwani wa Kata ya Zuzu, Awadh Abdallah

Pongezi hizo zilitolewa na Diwani wa Kata ya Zuzu, Awadh Abdallah nje ya ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Diwani Abdallah alisema kuwa miradi ya ujenzi wa madarasa mapya, visima vya maji na barabara za lami inakwenda sambamba na malengo ya serikali ya kuhakikisha huduma bora kwa wananchi. Miradi hiyo imeanza kutoa matokeo chanya na wananchi wanaendelea kunufaika nayo.

"Kwanza tunatekeleza mradi mkubwa wa Kituo cha Afya Zuzu kitakachogharimu shilingi milioni 550 na mpaka sasa takribani shilingi millioni 320 tumeshazipokea na ujenzi unaendelea. Tumejenga madarasa nane, matundu 16 ya vyoo na ofisi za walimu kwa ajili ya kidato cha tano na sita ambao tunatarajia mwaka unaofuatia tutaanza kuwa na wanafunzi wa kidato cha tano na sita.

"Lakini pia tunajenga shule mpya ya msingi katika Mtaa wa Soweto, mpaka sasa madarasa matano yamekamilika na tunaanzisha Shule ya Sekondari Chididimo. Kwahiyo, kutakuwa na shule nyingine ya Sekondari katika mitaa miwili ambayo ni Sokoine na Chididimo. Tayari tumeshaweka kwenye bajeti ya mwaka 2024/2025 katika utekelezaji” alisema Abdallah.

Akiongelea mradi mkubwa wa maji, alisema kuwa mradi huo unasimamiwa na Mamlaka ya Maji safi na usafi wa Mazingira mjini Dodoma (DUWASA) ukitarajiwa kuchimba visima 13. Visima vitatu vimeshachimbwa na mradi utasaidia kusambaza maji hadi kata za jirani, aliongeza.

Aidha, Diwani huyo alitoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwapelekea mradi wa barabara ya lami katika kata hiyo. “Tunamshukuru sana Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 13 na utekelezaji umeshaanza kwa kilomita sita na nusu na umefikia asilimia 50 na mpaka mwezi wa Oktoba hizi kilomita zitakuwa zimeanza kutumika” alisema Abdallah.

Abdallah alizitaja fursa zinazopatikana kwenye kata yake kuwa ni bwawa la Zuzu ambalo hutumika kupata kitoweo na umwagiliaji. Vilevile, alisema kuwa kuna mashamba yanayofaa kwa kilimo cha mjini.

“Nitoe fursa ambazo zipo kwenye kata yetu. Kwanza ni karibu na mjini, tumeanza upimaji wa ardhi na sasa wananchi wananufaika na ardhi yao. Lakini pia tumepata wafadhili wa 'World Bank' ambao watakwenda kupima ardhi kwenye mitaa mitatu ambayo ni Sokoine, Soweto na Chididimo kwa gharama nafuu kwa ajili ya wananchi kuweza kumudu gharama za uendeshaji.

"Pia tuna bwawa kubwa unaweza kunufaika kwa samaki, kilimo cha mbogamboga na tuna viwanja ambavyo tunaviuza vya hoteli na mashamba. Kwahiyo, tunawakaribisha sana kwa hizi fursa zinazopatikana kwenye Kata ya Zuzu” alisema Abdallah.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma